Saturday, 10 December 2016

makamu wa rais kuzindua mpango kazi wa kutokomeza ukatili

miwaniii
S.NKINGA: MPANGO KAZI WA TAIFA WA KUTOKOMEZA UKATILI DHIDI YA WANAWAKE NA WATOTO KUZINDULIWA TAREHE 13/12/2016
Na erasto ching’oro– Mkuu wa Kitengo cha Mawasiliano, Wizara ya Afya, Maendeleo ya jmaii, jinsia, wazee, na Watoto
Tarehe 13, Desemba 2106 Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano ya Tanzania Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan, atazindua Mpango Kazi wa Taifa wa Kutokomeza Ukatili Dhidi ya Wanawake na Watoto, shughuli itakayofanyika katika Ukumbi wa Kimataifa wa Julius  Nyerere,  Dar es Salaam.
Katibu Mkuu wa Wizara ya Afya Maendeleo ya Jamii, Jinsia, wazee na Watoto Sihaba Nkinga, ambaye Wizara yake ndio inyoratibu Uzinduzi huu anabainisha kuwa, Mpango Kazi wa Kutokomeza Ukatili Dhidi ya Wanawake na Watoto unalenga kushirikisha Serikali na wadau wengine katika jitihada jumuishi za kuzuia ukatili dhidi ya wanawake na watoto na hivyo kusaidia wahanga wa ukatili kupata huduma stahiki ili kudhibiti ukatili nchini.
Kumekuwepo na matukio mengi ya ukatili yanayosababishwa na mambo mbalimbali ikiwa ni pamoja na umaskini katika familia, mila na desturi potofu zenye athari katika jamii, malezi na makuzi mabovu na sheria kandamizi. Katibu Mkuu S. Nkinga anatanabaisha kwamba, kabla ya kuandaliwa kwa Mpango Kazi huu, Tanzania ilikuwa na mipango kazi minane (8) ya kuzuia ukatili dhidi ya wanawake na watoto. Mipango hiyo ilikosa uratibu wa pamoja na hivyo kushindwa kuleta matokeo makubwa katika kutokomeza ukatili.
Aidha, ameongza kuwa mipango hiyo haikuwa na mfumo wa pamoja wa kufuatilia na kutathmini ufanisi unaopatikana. Vilevile, kutokana na madhara ya ukatili dhidi ya wanawake na watoto katika maendeleo ya nchi wanachama wa Umoja wa Mataifa, wakuu wa nchi wanachama waliazimia kwa pamoja kutokomeza ukatili huo kupitia utekelezaji wa lengo Na. 5 na 6 ya Malengo ya Maendeleo Endelevu ifikapo 2030.
Itakumbukwa kuwa, Tanzania ni kati ya nchi nne (4) za kwanza duniani na nchi pekee katika Afrika iliyowezeshwa kupitia jukumu lilioanzishwa la kusaidia nchi wanachama wa Umoja wa Mataifa kuandaa mpango wa kuzuia na kuitikia afua za kudhibiti ukatili ili kuwa na mipango thabiti ya upatikanaji wa haki, usawa na maendeleo kwa wote.
Akieleza katika kikao na waandishi wa Habari mapema wiki hii, Katibu Mkuu Nkinga aliseama kuwa Mpango kazi huo wa aina yake una maeneo makuu manane (8) yatakayotekelezwa na wadau wa maendeleo ya wanawake na watoto. Meneo hayo ni Uimarisha  wa uchumi wa kaya; Uzuiaji wa mila na desturi zenye madhara; na Uboreshaji wa mazingira salama katika jamii.
Maeneo mengine ni Kuendeleza mazingira salama ya mafunzo shuleni na stadi za maisha na kuhuisha mahusiano, malezi na makuzi katika familia; Utekelezaji na usimamizi wa sheria; Utoaji huduma kwa wahanga na mwisho, ni sehemu ya Uratibu, ufuatiliaji na tathmini ya utekelezaji wa mpango kazi wa miaka mitano kuanzia mwaka 2017/2018 hadi 20121/21022.
Mpango Kazi huu mahususi unatarajiwa kuwa na matokeo makubwa baada ya miaka mitano ya utekelezaji kwani utawezesha kuondoa ukatili dhidi ya wanawake kwa asilimia 50 kufikia mwaka 2021/2022; na Kuondoa ukatili dhidi ya watoto kwa asilimia 50 kufikia mwaka  2021/2022, na hivyo kuleta mabadiliko makubwa kwa kuwa na familia salama, na jamii yenye utulivu.
Mwisho, Katibu Mkuu Nkinga, anaeleza kuwa, Mpango Kazi wa Taifa wa Kutokomeza Ukatili Dhidi ya Wanawake na Watoto nchini Tanzania utakuwa ndiyo dira kwa wadau wote wa masuala ya maendeleo ya wanawake na watoto hapa nchini. Mpango unabainisha kazi zitakazotekelezwa na kila mdau kuanzia familia, jamii, halmashauri, mikoa, wizara za sekta, sekta binafsi, asasi za Kiraia na wabia wa maendeleo. Mpango umeweka mfumo fungamanishi wa uratibu, ufuatiliaji na tathmini. Aidha, mpango utaratibiwa katika ngazi ya Taifa na Ofisi ya Waziri Mkuu, ngazi ya mikoa na Makatibu Tawala wa Mikoa, na ngazi ya halmashauri na Wakurugenzi Watendaji.
Mwisho, Wizara inawahimiza washiriki wote waliopata mwaliko kuhakiksha kuwa wanafika mapema katika mkutano huu muhimu. Vile vile, Wizara inatoa rai kwa vyombo vya Habari kutoa ushirikiano katika kutangaza tukio hili la uzinduzi wa Mpango Kazi wa Kutokomeza Ukatili, na pia kuwaelimisha wananchi waweze kuuelewa mpango huu ili kuongeza uelewa wa wadau na jamii na kuwa tayari kuzuia ukatili wa kijinsia na kutoa huduma kwa wahanga.

No comments:

Post a Comment