UKABILA NI DHAMBI

 


UKABILA NI DHAMBI YA UBINAFSI NA UBAGUZI LAKINI  INAYOLINDWA KWA NGUVU NYINGI SANA
Siku moja nikiwa shuleni miaka ya mwanzoni  mwa themanini  namkumbuka Mwalimu wangu mmoja Ndugu. Nsapaje aliyekuwa akitufundisha somo la siasa alipomtandika bakora mwenzetu mmoja kwa kumuita mwenzie kwa kabila lake. Nkana alimuita Mariam “we Mbungu unaitwa!” (wabungu ni moja kati ya makabila zaidi ya nane yanayopatikana mkoani Mbeya katika Wilaya ya Chunya. Pasipo kutambua kwamba nyuma yake alikuwa Mwalimu Nsapaje anajongea darasani. Mwalimu Nsapaje alichukia sana watu kuitana, kuulizana wala kutambulishana kwa kutumia makabila yao. Alisema hiyo ni dhambi mbaya sana na haipaswi kuvumiliwa.

Alimkamata Nkana na kuingia naye darasani huku akiwa amefura hasira. Mbele ya darasa akamwita Mariam pia na kumwambia Nkana arudie alichomtamkia mwenzie. Kwa kutambua kosa alilolifanya Nkana alisita sana kuirejea kauli yake. Hata hivyo mwalimu hakumuacha mpaka alipotamka kauli ile na kukiri mbele ya darasa.

Mariam alionekana amenyongea sana, amekosa raha kwa kile alichoambiwa na Nkana. Alijiuliza maswali mengi sana kwamba pengine hastahili kuwapo Tanzania, labda ni mkimbizi na mengine chungu mzima. Lakini alifarijika sana kwa kuwa Mwalimu alisikia moja kwa moja ingawaje pia yalikuwa makusudi yake pia aende kushtaki kwa Mwalimu wa Nidhamu yaani Mwalimu Nsapaje.

Baada ya Nkana kukiri mbele ya darasa, Mwalimu Nsapaje akaligeukia darasa zima na kuuliza:-
Mwalimu:  ni nini kosa hapo?,
Wanafunzi:  ametenda dhambi ya Ubinafsi na Ubaguzi
Mwalimu: Adhabu yake nini?
Wanafunzi: Viboko kumi na viwili, kufyatua tofali na barua ya onyo
Mwalimu: Akirudia tena adhabu gani?
Wanafunzi: Afukuzwe shule

Kwa wakati ule shule yetu ilikuwa na sheria kali sana dhidi ya waliofanya dhambi ya ubaguzi kwa wenzao, waliogombana ama kutumia lugha chafu dhidi ya wenzao na kadhalika. Walimu wote, Wazazi  na wanafunzi walikuwa wasimamizi wa sheria zilizowekwa. Tuliogopana kwa wema na hatukuaminiana kwa wema. Mambo yakawa safi.

Nilipoanza kuandaa CV kwa ajili ya kazi na hata sasa naogopa sana kujitambulisha  Kabila na Dini yangu  nikiamini kwamba ni ubaguzi na ubinafsi wa hali ya juu ambao pia haunisaidii chochote katika kupata kazi zaidi ya kuchangia katika kufanikisha nia ovu ya ubinafsi na ubaguzi wa kiwango cha juu sana katika ajira hasa pale muajiri anapokuwa hajitambui wala kutambua majukumu yake sawasawa.

Kuanzia miaka ya mwanzoni mwa 2000 mpaka sasa nimekuwa katika nafasi ya kusimamia raslimali watu sehemu mbalimbali katika sekta ya hoteli. Moja kati ya miiko yangu mikubwa ni kutotoa ajira kwa misingi ya ukabila, udini na wala aina yoyote yenye mlengo ama harufu ya rushwa. Ninashukuru nimefanikiwa katika hilo kwa kiwango kikubwa. Miongoni mwa watakaoisoma makala hii ni watu niliofanya nao ajira ama kuhusika katika zoezi lao la usaili na hapana shaka watakuwa mashahidi wangu wazuri katika hili. Naogopa sana Ukabila na Udini kama nilivyofundishwa na Mwalimu wangu Nsapaje.

Nikiwa mtu mzima nikaendelea kuuona ukweli wa Mwalimu Nsapaje ambaye alipendelea kuingia shuleni akiwa na mavazi ya JKT wakati huo na kunifanya niamini sana kwamba askari yoyote ndiyo kielelezo cha Uzalendo. Ninamkumbuka Mwalimu wangu sana hasa alipoongelea suala la kutokuwa wabinafsi na wabaguzi, niliiona kauli yake ikiwa imetoka moyoni haswa na wala haikuwa ya kinywani peke yake. Wako wapi akina Mwalimu Nsapaje wengine leo?, waliishia wapi?, hawakuacha urithi?. Najiuliza maswali haya lakini nakosa majibu sahihi.

Leo ninapoandika walaka huu ninaiona dhamira y dhati ya Mwalimu Julius Kambarage Nyerere, Baba wa Taifa la Tanzania kuamua kutuunganisha kwa lugha moja tu yaani KISWAHILI. Najaribu kuitafakari Tanzania ya leo hii bila kuwapo na lugha inayotuunganisha. Kila mtu katika makabila yetu zaidi ya mia moja na ishirini angekuwa anatumia lugha yake katika mawasiliano sijui nini kingetokea.

Moja ya hotuba muhimu sana kwa Taifa la Tanzania zilizowahi kutolewa na Baba wa Taifa ni ile aliyoitoa katika Mkutano Mkuu wa Chama cha Mapinduzi 1995 wakati wa mchakato wa kumpata mgombea urais wa serikali ya awamu ya tatu. Mwalimu alitaja mambo manne kuwa yanahitaji rais atakayekuwa tayasimamia kwa dhati ya moyo wake. Rushwa, Umaskini, Udini na Ukabila mwalimu aliona vimeanza kuota mizizi hapa nchini wakati huo lakini kwa sasa sio tu vina mizizi bali vimeanza kuzaa matunda. Kwa faida ya wasomaji wangu nitainukuu hotuba yote.


 HOTUBA YA MWALIMU JULIUS KAMBARAGE NYERERE ALIYOITOA KATIKA MKUTANO MKUU WA CCM MWAKA 1995 MJINI DODOMA
 “Rais amewaambieni na mimi nasisitiza, nitamalizia hapo sitaki kuchukueni  muda wenu mrefu. Teueni mgombea ambaye atakidhi matarajio ya Wananchi, acha matarajio yako wewe mpiga kura. Tupeni mgombea ambaye atakidhi matarajio ya Watanzania.
Watanzania wanataka mabadiliko, wasipoyaona, wasipoyapata ndani ya CCM watayatafuta nje ya CCM. Watanzania kuna mambo wanataka uongozi wa awamu ya tatu uyafanye, mengi tu mimi nitataja machache. Mengi tu lakini nitataja machache, yatawatosheni.
La kwanza, nitataja manne, la kwanza; Watanzania wamechoka na Rushwa. Wajumbe wa zamani wa Halmashauri kuu ya Taifa watakumbuka nimelipigia kelele suala la Rushwa ningali Mwenyekiti wao hapahapa Dodoma. Nilipiga kelele kiasi kwamba Waziri Mkuu wa wakati huo alikwenda kwa Rais, alikuja kwako Ndugu Rais kuja kutoa hati yake ya kujiuzulu. Sasa hivi hali ya Rushwa ni mbaya zaidi nchini, wasaidieni wananchi ku-deal nayo. Mgombea mtakayemteua lazima tumtetee, wote tumtetee. Lakini inatakiwa ukiulizwa swali, huyu atatusaidia kupiga rushwa vita?, jibu litoke ndani ya roho yako hapana hapa tu (mdomoni) kwamba ndiyo anaweza. La kwanza.
La pili; nchi yetu masikini, nchi yetu hii masikini. Wakulima wetu, wafanyakazi wetu masikini. Nchi hii bado ni nchi ya wakulima na wafanyakazi ambao wote ni watu masikini. Nchi hii haijawa ya matajiri, Chama hiki hakijawa chama cha matajiri!. Tunataka tuendelee kushughulika na umasikini wa watu wetu,tushughulike kwa dhati na matatizo ya wananchi ya uchumi wao, Hali yao ya uchumi, hali yao ya viwandani, hali yao ya mashambani, hali yao ya shuleni, hali yao ya hospitalini. Tunataka kuwa na hakika kwamba mtatuteulia mtu ambaye ukiulizwa swali huyu anajua?, kwamba nchi hii ni nchi bado ni nchi ya masikini?, kwamba nchi hii bado ni nchi ya wakulima na wafanyakazi, anajua hivyo?. Uweze kumjibu Yule anayekuuliza hivyo kwa moyo wa dhati kwamba Naam!, huyu anatambua hivyo.
Sasa hivi katika nchi yetu, la tatu, nataja la tatu, watu wameanza kutuzungumzia udini, tulikuwa hatuzungumzi mambo ya udini udini katika nchi hii, hata kidogo. Tulikuwa hatujali dini ya mtu, anaijua mwenyewe dini yake, basi. Ilikuwa haiji katika akili yetu kwamba tunapompima mtu tumchague huyu tumfanye rais au tumfanye nani tunauliza dini yake, hatuulizi hata kidogo, tulikuwa hatuulizi hata kidogo. Dini inatuhusu nini sisi?. Zamani katika kuhesabu watu hapa Tanzania, katika kuhesabu watu wakati wa mkoloni, siku ya sensa swali lilikuwa linauliza dini ya mtu. Tukasema sisi hatujengi misikiti, hatujengi makanisa, hatujengi mahekalu hili swali la udini ya mtu tunaliuliza kwa nini?. Linatuhusu nini?, tunataka kujua umri wa watu, kwa sababu hiyo ina maana, tunataka kujua kama watu wanajua kusoma na kuandika hiyo ina maana, tunataka kuuliza mambo ambayo serikali inayataka. Kama maimamu wanataka kuuliza, wanataka kujua wana Waislamu wangapi watafute wao sisi inatuhusu nini?, kama maaskofu wanataka kujua wana Wakristo wangapi watafute wao si wanakuja makanisani kuungama?, wawaulize!. Sisi inatuhusu nini jambo la dini hata tuulize watu wewe dini yako nani, inatuhusu nini sisi?. Hiyo ndiyo ilikuwa Tanzania tunayojaribu kuijenga.Sasa watu wanazungumza dini, udini bila haya, bila aibu. Wanajitapa kwa udini!. Tunataka mtuchagulie mgombea ambaye atatusaidia kuondoa mawazo haya ya Kipumbavu katika nchi yetu. Na ukiulizwa na wananchi wa Tanzania kwa dhati, mnadhani mgombea huyu analiona hilo kwa uchungu kama mnavyoona nyinyi mseme ndiyo, uweze kujibu kwa dhati kabisa kwamba Ndiyo.
La mwisho, nilisema nitataja manne tu. Nilikuwa New York mwaka jana, yupo mwenzenu mmoja Getrude Mongela, sasa hivi ni Katibu wa akina mama wa Mkutano wa akina mama utakaofanyika Beijing. Gaetrude alinikaribisha chakula jioni katika flat yake hapo New York, akakaribisha jamaa wengine nikaonana nao pale. Wakati tunakula, mama mmoja wa Kiganda ambaye anafanya kazi hapo kanambia Mzee mimi nilikuwa nafanyakazi katika jumuiya ya Afrika ya Mashariki. Wakati nafanya kazi katika jumuiya ya Afrika ya Mashariki, sisi watu wa Uganda tulikuwa tunajuana kwa makabila yetu, na tunatajana kwa makabila yetu. Watu wa Kenya walikuwa wanajuana kwa makabila yao, huyu Mkikuyu, huyu Mjaluo, huyu Muruya na wanatajana kwa makabila yao. Watu wa Tanzania walikuwa kabisa kabisa hatujui makabila yao. Nilimwambia Yule mama ni wakati huo mama!, nilimwambia ni wakati huo sio sasa. Sasa Watanzania wanaanza kuulizana makabila, wanafikiri ni jambo la maana sana kujua kabila la mtu, mnataka Kutambika?. Maana faida ya makabila iliyobaki ni kutambika tu, basi!, lakini hasa ina maana gani nyingine?. Katika nchi ya watu wazima, kabila lina maana gani nyingine?. Tukifanya mitambiko pale Butiama pale tunafanya, mimi nipo karibu pale na chaka letu ambapo ndipo  mungu wa Watiama wale anakaa. Lakini kabila hasa, Tanzania ya leo inazungumza Kabila!!. Wazungu wale waliotutawala wana Mataifa makubwa makubwa, yametawala dunia. Leo wanaviona vitaifa vyao vile ni vidogo mno wanaungana. Waingereza na jeuri yao yote wametawala dunia, Wafaransa na jeuri yao yote wametawala dunia, Wajerumani  na jeuri yao yote wameipiga Ulaya. Leo wanaungana kuwa Taifa moja. Nyinyi Waswahili, vinchi vidogovidogo hivi, vya watu ishirini na saba milioni mnazungumza makabila!!, mnazungumza lugha ya makabila!!, mtuingize katika karne ya ishirini na moja mnapanda basi la makabila!!. Lakini tumeanza kuzungumza ukabila. Tunataka mtuchagulie mtu ambaye anajua kwamba huko ni Upumbavu na ni hatari huko.Hatuwezi, lugha ya ukabila hatuwezi kuzungumza. Wenzetu wanatushangaa, wenzetu majirani sisi ndiyo ilikuwa mfano wao mbona Tanzania hawazungumzi ukabila sisi tunazungumza ukabila, mfano wao ulikuwa ni Tanzania. Tunataka kuwaiga majirani zetu katika hilo?. Tunataka kusema Kenya wanazungumza makabila na sisi tusizungumze ukabila kwa nini?, Tunasema Uganda wanazungumza makabila na sisi tusizungumze ukabila vilevile kwa nini?, Tunasema Rwanda na Burundi wanazungumza makabila na sisi tuzungumze ukabila, tunasema hivyo Watanzania??!!, bila haya?. Kabila si jambo la kuonea haya, kabila linakuwa ni jambo leo unaweza kusema katika basi unajitapa ukabila!!?. Tunataka mtuteulie kiongozi anayejua hiyo, atusaidie.
Ndugu Wananchi, Ndugu Mwenyekiti, Mimi mliniomba nije kusaidia, nilikubali kuja kusaidia, kwa nini? Kwa sababu hiyohiyo. Tunataka nchi yetu ipate Kiongozi safi, Kiongozi safi hawezi kutoka nje ya CCM.
Nyinyi wapiga kura mnaweza kutupatia kiongozi safi kwa kura zenu, basi tupatieni kiongozi safi kwa kura zenu.
 Ahsanteni sana!”.
Pamoja na mengi ambayo Mwalimu Nyerere aliyasema kwa kuonya enzi za uhai wake tukayapuuza leo hii tunaona madhara yake katika jamii zetu. Hata hivyokatika waraka huu tutatazama zaidi suala la “UKABILA” jambo ambalo aliliongelea kwa uchungu sana.

VIASHIRIA VYA UKABILA
Katika nchi yetu kwa sasa tunavyoviashiria vingi sana vya ukabila lakini ninashawishika kuyaona mambo mawili katika uwepo wake na kuenea kwake katika jamii kwa sasa.
a)      Wengine wanafanya kwa kuiga na huku wakidhani ndiyo uzalendo kwa makabila yao
b)      Wengine wanafanya huku wakijua fika kitakachovunwa hapo baadaye lakini wanaongozwa na Ubinafsi na Unafiki.

Kufanya Kwa kuiga:                                                                  
Yapo mengi sana tuliyoyaiga kwa kudhani ndiyo kwenda na wakati pasipo kuchukua muda wa kutafakari kwa kina kujua upande hasi na upande chanya wa kile tunachoiga. Hali hii mara nyingi imepelekea kumomonyoka kwa maadili na kusababisha matatizo makubwa katika jamii zetu. Mbaya kuliko yote ni pale tunapoiga mabaya mengi kuliko mazuri ambayo siku moja tungeweza kusimama hadharani na kujivunia.

Vyama vya kikabila vya kufa na kuzikana vimeendelea kutamalaki sana nchi kwetu na hasa kwa takribani miongo hii mitatu. Mlango huu wa ukabila unainuka kwa kasi ya ajabu kwa tiketi ya kusaidiana wakati wa misiba. Swali la msingi hapa ni kwamba kwa nini tunataka kusaidiana wakati wa kutoka kwa uhai wa mtu?. Jibu rahisi ni Ubinafsi na Unafiki.

Pamekuwepo na mtindo wa watu kujipatia umaarufu kupitia shughuli kubwa kubwa na hasa zinazogusa jamii kwa ukaribu sana kama misiba. Gharama kubwa sana watu wamekuwa wakizitumia katika mazishi ya wapendwa wao kuliko zile ambazo zingepaswa kutumika kwa mfano katika kumuuguza mgonjwa kabla ya kufa kwake. Utafiti unaonyesha kwamba watu hutoa michango mikubwa mikubwa katika misiba kuliko katika ugonjwa wa mtu. Unamsaidiaje mtu na inakusaidia nini wewe unayetoa kwa sifa msibani lakini hukujali wakati pakihitajika gharama za matibabu. Ili kudhirisha kwamba vyama vya ukabila katika suala la msiba havina maana yoyote bado tumeendelea kuona ushiriki wa jumla wa wale wasiokuwa wa kabila hilo kuliko hata kwa wenye kabila. Pia pameendelea kuwapo manung`uniko katika sehemu nyingine kwamba vyama hivyo hivyo vya ukabila vimekuwa na ubaguzi wa hali ya juu baina ya walionacho na wasionacho.

Watu wengi sana wamekuwa wakiiga mitindo hii ya vyama vya kikabila hata pasipo kufanya uchunguzi wa kina kubaini faida na hasara zake. Kwa tafsiri ndogo tuliyonayo tunadhani tunafanya kama mtindo madhubuti wa kujiimarisha katika kabila letu. Lakini tujiulize, yote haya na kwa faida ya nani?. Kabila lako liisha kuimarika lishindane na nani katika nini?.

” Nilimwambia Yule mama Ni wakati huo mama!, nilimwambia ni wakati huo sio sasa. Sasa Watanzania wanaanza kuulizana makabila, wanafikiri ni jambo la maana sana kujua kabila la mtu, mnataka Kutambika?. Maana faida ya makabila iliyobaki ni kutambika tu, basi!, lakini hasa ina maana gani nyingine?. Katika nchi ya watu wazima, kabila lina maana gani nyingine?”.

Ingelikuwa jambo la maana sana kama Watanzania wangeamua kuanzisha mshikamano wa kimitaa ambao baadaye unatengeneza nguvu kubwa ya Taifa. Hebu tujiulize haya yafuatayo kasha tuweke kwenye mzani tuuone uzito uko wapi kati ya mshikamano wa Kitaifa na mshikamano wa kikabila.

Mosi;     a). Ni nani kati yetu ambaye mtaani kwake pamekosekana maendeleo kwa sababu anaoishi nao                                 sio wa kabila lake?.
b). Ingelikuwaje kama wakazi wa mtaa Fulani wamkaamua kuweka makabila yao kando na       badala yake waijenge jamii ya mtaa wao kimaendeleo?

Pili;         a). Ni nani ambaye akipatwa na tatizo wanahusika watu wa kabila lake pekee kwa sababu ya chama cha kabila lake?
c)       Kama wakazi wote wanaweka kando makabila yao wakati mwenzao akiwa na tatizo, ni wapi unaonekana umuhimu wa kuwa na chama cha kikabila.

Ukabila hauna zaidi ya ubinafsi, ubaguzi na unafiki uliotukuka ambao katu hauwezi kutetewa kwamba umewahi kuwa na tija ama manufaa yoyote zaidi ya kila mtu kujipambanua kwamba wanalo kabila. Makabila yametutafuna hata katika taasisi zetu za kidini. Watu wamepigana na kushutumiana kwa misingi ya ukabila pasipo hata kuangalia kwamba dhehebu husika halihitaji uwepo wa kabila kwa kuwa linahudumia watu wa makabila na rangi zote.

Dhambi ya ukabila ni kubwa sana kwani hata mifumo yetu ya kiutawala katika nchi imeingiliwa na ubinafsi, ubaguzi na unafiki na hivyo kufanya ukabia utamalaki. Vigezo vya msingi katika ajira vimewekwa kando na sasa watu wanaajiriwa kwa makabila yao. Taifa linaangamia, hakuna uzalendo tena, hakuna uwajibikaji tena, hakuna tija katika uzalishaji, hakuna uadilifu maofisini, viwandani na mashambani. Migogoro ya wakulima na wafanyakazi ni ukabila tu, ujinga unaoendelea kwenye siasa zetu ni ukabila tu, kukosekana kwa maamuzi sahihi ni ukabila tu, kudorola kwa maendeleo ya kiuchumi ni ukabila tu.

Tamaa ikichukua mimba huzaa dhambi, dhambi ikiisha kukomaa huzaa mauti. Watu wanayatamani makabila yao zaidi kuliko Taifa lao na sasa tama zao zikazaa dhambi ya ubaguzi, ubinafsi na unafiki. Dhambi hiyo imeendelea kukomaa na mpaka sasa zipo dalili za kutosha kabisa kwamba dhambi hizo zimekomaa kiasi cha kuelekea kuzaa mauti.






Soma zilizopita

No comments:

Post a Comment