Wednesday 31 August 2016

Waziri aliyesinzia mkutanoni auawa Korea Kaskazini

 Rais Kim Jong-un na mkewe Ri Sol-ju

Serikali ya Korea Kusini imesema waziri wa elimu nchini Korea Kaskazini ameuawa na maafisa wa serikali.
Waziri huyo wa elimu Kim Yong-jin anadaiwa kusinzia katika mkutano wa kiongozi wa nchi hiyo Kim Jong-un.
Baadhi ya ripoti zinasema waziri huyo, ambaye amekuwa pia akihudumu kama mmoja wa manaibu wa waziri mkuu, alitekwa na usingizi wakati wa mkutano huo jambo ambalo lilichukuliwa kama kumkosea heshima kiongozi huyo.
Maafisa wa Korea Kusini wamesema wanaamini waziri huyo aliuawa kwa kupigwa risasi mwezi Julai.
Serikali hiyo inasema maafisa wengine wawili walilazimishwa kwenda kuishi maeneo ya mashambani, "kupewa upya mafunzo".

Korea Kusini iliwahi kutoa taarifa kwamba kiongozi wa jeshi la Korea Kaskazini Ri Yong-gil alikuwa ameuawa mwezi Februari mwaka huu.

Lakini mwezi Mei mwaka huu, ilibainika kwamba alikuwa bado hai na alikuwa akihudhuria mikutano na hafla rasmi za serikali.

Mara ya mwisho Korea Kaskazini kutangaza hadharani kwamba ilikuwa imemuua afisa mkuu serikalini ilikuwa ni mwaka 2013 wakati mjombake rais wa nchi hiyo, Chang Song-thaek aliuawa mwaka 2013.

Tangazo la kifo cha Kim Yong-jin limetolewa na wizara ya muungano ya Seoul na limetolewa siku chache baada ya taarifa za gazeti moja kusema maafisa wawili wakuu wa Korea Kaskazini waliuawa kwa kulipuliwa kwa makombora ya kutungua ndege.

Gazeti hilo lilisema wawili hao waliuawa mapema mwezi huu.

Watu zaidi ya kumi wameuawa tangu Kim Jong-un achukue hatamu miezi mitano iliyopita.

Baadhi ya wachanganuzi wa masuala ya siasa wanasema huenda kiongozi huyo, mwenye umri wa miaka 32, hutumia njia ya kuwaua watu hadharani kusisitiza udhibiti wake kama kiongozi.

Waziri huyo alichunguzwa baada ya kusinzia mkutano wa Rais Kim Jong-un

Mapema mwezi huu, naibu balozi wa Korea Kaskazini nchini Uingereza aliikimbia nchi yake na kuhamia rasmi Kusini.

No comments:

Post a Comment