Monday 29 August 2016

Mwanasheria Mkuu wa Serikali avionya vyama vya siasa

  Image result for GEORGE MASAJU
Mwanasheria Mkuu wa Serikali George Masaju aonya vyama vya siasa kutumia maneno yanayovunja amani na usalama wa nchi.
Masaju ambaye amezungumza na wahariri wa vyombo vya habari jijini Dar es salaam leo, ametolea mfano Oparesheni UKUTA iliyotangazwa kufanywa na CHADEMA na kusema kuwa ina maneno ya kijeshi yanayotumiwa kwenye shughuli za kihalifu.


Amesema neno UDIKTETA siyo sahihi kwa kuwa nchini Tanzania hakuna udikteta kwa kuwa serikali inafanya shughuli zake kwa mujibu wa sheria na nchi inaendeshwa kwa kuzingatia mgawanyo wa madaraka wa katika miimili yote mitatu ya dola.

“UKUTA lengo lake ni nini, ni sawa na kuwatenganisha wananchi na serikali yao” Amesema Masaju na kuwataka wananchi kutambua kuwa Septemba Mosi ni siku ya Majeshi nchini huku akishangazwa na CHADEMA kuchagua siku hiyo kuzindua kampeni yao aliyodai kuwa ina lengo la kuvuruga nchi.

Masaju amewataka viongozi wa vyama vya siasa nchini kutii mamlaka za dola ikiwemo Jeshi la Polisi na mahakama iliyowapa mwongozo juu ya ombi la kupinga zuio la jeshi la polisi na pia kufuata ushauri waliopewa na Tume ya Haki za Binadamu na Utawala Bora juu ya kutokuwepo kwa udikteta nchini.

Amesema sababu kuu za kuzuia Oparesheni ni mbili ambazo ni hali ya usalama kutokuwa shwari, pamoja na kutokuwepo kwa udikteta nchini.

No comments:

Post a Comment