Thursday 28 April 2016

Serikali kupata Maoni ya Wananchi Kuhusu Marekebisho ya Sheria ya Ndoa na kutungwa kwa Sheria Mpya ya Mirathi na Urithi

 
 
 
 Na Mwandishi wetu

Serikali   imejiandaa kuleta Muswada wa Sheria bungeni kutoa haki ya kusoma kwa watoto wote wa kike na kiume wa shule za msingi, sekondari Na kutoruhusiwa kuoa au kuolewa.

Aidha, Waziri wa Katiba na Sheria, Dk Harrison Mwakyembe amesema Serikali inaendelea kukamilisha utaratibu wa kupata maoni ya wananchi kuhusu marekebisho ya Sheria ya Ndoa na kutungwa kwa Sheria mpya ya Mirathi na Urithi kuondokana na mkanganyiko uliopo kuhusu sheria hiyo.

Bunge lilielezwa hayo jana mjini Dodoma wakati waziri huyo akijibu swali la Nyongeza la Mbunge wa Ileje, Janeth Mbene (CCM) aliyehoji ni lini serikali itaanza maandalizi ya kuchukua maoni juu ya kufanya marekebisho sheria ya ndoa ya mwaka 1971.

Akijibu swali hilo, Dk Mwakyembe alisema hatua za awali zimeshaanza kuchukuliwa na wizara hiyo ili kupata maoni ya wananchi juu ya Marekebisho ya sheria hiyo ya ndoa ya mwaka 1971 na kutungwa kwa sheria mpya ya mirathi na urithi.

Alisema serikali ina nia ya dhati ya kufanyia marekebisho sheria ya ndoa na kwamba mchakato huo ulisitishwa kwa kuwa Tume ya mabadiliko ya Katiba ilikuwa ikikusanya maoni kuhusu mabadiliko ya katiba , hivyo walidhani Wananchi wangetoa pia maoni juu ya sheria hiyo.

No comments:

Post a Comment