Na Masanja Mabula -Pemba
Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed
Shein ameiagiza Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Amali kuangalia upya na
kwa mapana yake mahitaji, huduma na maeneo ya kujenga dhakhalia kwa
ajili ya skuli za sekondari na vyuo.
Dk.
Shein amesema serikali imedhamiria kuimarisha ujenzi wa dakhalia katika
vyuo kwa kuwa zina mchango kubwa sio tu katika kuimarisha masomo bali
hata kujenga mshikamano miongoni mwa wanafunzi wanaotoka maeneo mbali
mbali ya Zanzibar.
Akizungumza
katika hafla ya uzinduzi wa dakhalia ya wasichana katika Chuo cha
Ufundi huko Kingeja,Wilaya ya Mkoani Mkoa wa Kusini Pemba jana, Dk.
Shein alieleza kuwa mara baada ya Mapinduzi ya mwaka 1964, Serikali
iliweka mkakati maalum wa kujenga na kuimarisha dakhalia kwa kuwa ndio
lilikuwa suluhisho la haraka la kuwapa fursa watoto wengi kutoka
mashamba kupata elimu.
Dk.
Shein alieleza kuwa serikali hivi sasa kwa kushirikiana na Chuo Kikuu
cha Taifa Zanzibar (SUZA0 ina mpango wa kujenga dakhalia ya kisasa
mithili ya ‘mji wa wanafunzi’ huko Tunguu, wilaya ya Kati,Unguja ambapo
wanafunzi wa vyuo jirani na SUZA wataweza kuishi katika dhakhalia hiyo.
“Katika
eneo hilo (la dakhalia) tutajenga maduka, viwanja vya michezo na kila
kitu muhimu kawa maisha ya wanafunzi” Dk. Shein aleleza.
Katika
hotuba yake hiyo, Dk. Shein alieleza kwa kirefu namna dhakhalia miaka
ya nyuma zilivyoweza kujenga urafiki, udugu na mshikamano kati ya
wanafunzi kutoka sehemu mbali za visiwa vya Unguja na Pemba
halikadhalika kuondoa tofauti zilizokuwepo kabla ya Mapinduzi ya mwaka
1964.
“Dakhalia
zilikuwa na mchango mkubwa katika kuondoa tofauti na kasumba
zilizopandikizwa na wakoloni dhidi ya wananchi…zilikuwa daraja muhimu la
kuwakutanisha na kuwaunganisha watu wa mashamba na mijini na baina ya
watu wa Unguja na Pemba” Dk. Shein alieleza.
Aliongeza
kuwa katika dakhalia hizo wanafunzi waliishi kwa kuheshimiana na
kusaidiana wakiwa kitu kimoja na hivyo kuung’oa kabisa ubaguzi na ndio
maana kuna uhusiano mkubwa kati ya watu wa Unguja na Pemba kutokana na
sera ya elimu iliyotilia mkazo kuchanganya wanafunzi kutoka visiwa hivyo
viwili.
Hata
hivyo, alibainisha kuwa mafanikio katika ujenzi wa skuli za sekondari
na vyuo katika maeneo mbalimbali ya Unguja na Pemba katika miaka ya
tisini yalipunguza idadi ya wanafunzi wanaohitaji kukaa dakhalia kwa
kuwa wengi walipata fursa za kuendelea na masomo yao katika maeneo
wanayotoka.
“Lazima
nikiri kuwa mafanikio haya ambayo yamepelekea kupunguza idadi ya
wanafunzi katika dakhalia yametunyima fursa muhimu ya kuimarisha
uhusiano baina ya wanafunzi wa sehemu mbali mbali za Unguja na Pemba”
Dk. Shein alieleza na kusisitiza kuwa serikali italiangalia upya suala
hilo.
Wakati huo huo,
katika hotuba yake hiyo Dk. Shein ameitaka Wizara ya Elimu na Mafunzo
ya Amali kuimarisha mtaala wa mafunzo ya ufundi ili wanafunzi
wanaomaliza vyuo hivyo waweze kujiajiri na kuajirika.
Dk.
Shein aliueleza uongozi wa Wizara hiyo kuwa amepata taarifa za kuwepo
malalamiko kutoka kampuni nyingi kutoka nje zinazofanyakazi za ujenzi
Zanzibar kuwa zinapata shida kuajiri mafundi wenye ujuzi, vyeti na uwezo
wa kufanya kazi za useramala.
“Hizi
si habari njema. Lazima tushirikiane katika kutatua changamoto hii,
hasa tukizingata Zanzibar ilikuwa inasifika kwa kuwa na maseramala
wazuri” Dk. Shein alisisitiza.
Dk.
Shein aliwahimiza wanafunzi wa vyuo vya ufundi kuongeza bidii katika
masomo yao ili watakapomaliza waweze kuamua ama kuajiriwa au kujiari na
kufafanua kuwa hivi sasa kuna mahitaji makubwa ya masomo ya ufundi
Tanzania nzima.
Katika
maelezo yake mafupi kumkaribisha mgeni rasmi, Waziri wa Elimu na
Mafunzo ya Amali Mheshimiwa Riziki Pembe Juma alikiri kuwa sekta ya
elimu ina changamoto nyingi lakini alieleza kutiwa moyo na jitihada
binafsi za Mheshimiwa Rais katika kushughulikia masuala ya elimu.
“Kila
unapokwenda na kuiangalia sekta hii ina changamoto nyingi lakini sisi
watumishi wa wizara tunapata faraja kuona kila wakati tuko nawe
kushughulikia changamoto hizo” alisema Waziri huyo.
Aliwataka
wanafunzi wa kike katika skuli hiyo ya ufundi kuongeza bidii baada ya
kupata dakhalia hiyo mpya na ya kisasa ambayo ina uwezo wa kuchukua
wanafunzi 72. Dk. Shein yuko kisiwani Pemba kwa ziara ya siku tano kukagua na kuhimiza shughuli za maendeleo.
No comments:
Post a Comment