Friday 25 November 2016

Dereva atoweka na mamilioni ya dola India

Mashine nyingi za ATM hazifanyi kazi nchini India
Polisi katika mji wa Bangalore kusini mwa India wanamsaka dereva mwenye gari ambalo hutumiwa kusafirisha pesa za kuwepwa kwenye mitambo ya ATM baada yake kutoweka na rupee milioni 9.2 ($134,000; £107,000) zikiwa kwa noti mpya za rupee elfu 2.
Dominic Selvaraj, anadaiwa kutoweka na gari hilo pale mwenzake alipoingia ndani ya choo cha benki kuenda haja.
Polisi wamesema gari hilo lilipatika limeegeshwa mjini Bangalore baadaye siku hiyo.
Mashine za ATM zimeshuhudia milolongo mirefu wa watu tangu noti za 500 na 1000 kupigwa marufuku kama njia ya kukabiliana na ufisadi.
Serikali imezindua noti mpya za rupee 500 na 2,000, lakini bado hazijaanza kuzunguka vyema kwenye mfumo wa pesa nchini humo na benki nyingi zinakabiliwa na uhaba wa pesa hizo mpya.
Afisa mkuu wa polisi Charan Reddy amemwambia mwandishi wa BBC Imran Qureshi kwamba Bw Selvaraj alikuwa ameajiriwa kama dereva wiki tatu zilizopita na kampuni ya usafirishaji wa pesa kutoka kwenye benki hadi mitambo ya ATM.
''Hakuondoka na bunduki ya mlinzi. Tumeunda vikundi vinne kumtafuta dereva huyo,'' Bw Reddy alisema.


Afisa wa polisi mwengine amesema ''gari hilo halikuwa na mtambo wa mawasiliano wa setilaiti wa kusaidia kuifuatilia".

Nchini humo kumeshuhudiwa visa kadha vya uhalifu tangu marufuku ya pesa za noti 500 na 1,000 kutangazwa wiki mbili zilizopita, ambazo zilikuwa ni asilimia 86 ya pesa zilizokuwa zinatumika.

Marufuku hiyo imeisababishia uchumi mkubwa wa India kukwama.
Watu wameambiwa wanaweza kuweka amana pesa au kubadilisha noti za zamani kwenye benki hadi tarehe 30 mwezi Desemba.

Waziri mkuu Narendra Modi aliyetangaza tangazo hilo lililowashtua wengi alipokuwa akiwahutubia taifa hilo, alisema uamuzi huo ulikuwa wa kukabiliana na walaji rushwa na walanguzi wa pesa.

No comments:

Post a Comment