Sunday 26 February 2017

Sitahudhuria hafla ya waandishi wa habari White House - Trump

Rais Trump ametangaza kuwa hatahudhuria hafla ya kila mwaka inayoandaliwa na chama cha waandishi wa habari wa Ikulu ya White House.
Hafula hiyo kwa kawaida huwavutia wageni mashuhuri, wanasiasa na waandishi wa habari.
Tangazo lake limetolewa juma moja baada ya Rais kuimarisha mashambulizi yake dhidi ya mashirika ya habari.
Kwa kawaida hafula hiyo ya kila mwaka ya White House hutoa nafasi kwa waandishi wa habari na Rais kusahau tofauti zao kwa muda.
Marais 15 wamewahi kuhudhuria hafula hii ya jioni ambayo huwavutia nyota wengi na imeendelea kwa zaidi ya miaka 100.
Hata hivyo uhusiano kati ya waandishi na Rais Trump umezorota kwa majuma machache yaliyopita.
Rais amewasema baadhi ya waandishi wa habari na taasisi wanazofanyia kazi kama habari bandia na kuwataja kama maadui wa wa Marekani.
Mnamo Ijumaa, Ikulu ya White House iliwafungia nje waandishi wa habari katika mkutano wa waandishi wa Rais. Miongoni mwa waliofungiwa nje ni CNN, New York Times pamoja na BBC.
Hafula hiyo ya jioni huzalisha habari za kitaifa lakini mwaka wa 2011 haukuwa mzuri wa Bwana Trump kwa sababu hafla hiyo ya chakula cha jioni, ilitoa nafasi kwa Rais Obama kumkebehi Bwana Trump kwa madai aliyokuwa ameyasambaza kila mahali kuwa Bwana Obama hakuzaliwa Marekani kwa hivyo hakustahili kuwa Rais wa taifa hilo.

Waandalizi wa hafula hiyo wamesema kuwa itaendelea na uhuru wa vyombo vya habari utapewa kipao mbele kulingana na Katiba ya Nchi.

No comments:

Post a Comment