Wednesday 27 July 2016

Mkuu wa mkoa wa Pwani mhandisi Evarist Ndikilo amezindua mpango mkakati wa kudhibiti ukimwi wa miaka mitano ijayo lengo likiwa kupambana na maambukizi mapya

indexMkuu wa mkoa wa Pwani mhandisi Evarist Ndikilo akionyesha kitabu cha taarifa cha mpango mkakati wa kudhibiti virusi vya ukimwi na ugonjwa wa ukimwi ,mpango ambao ni wa miaka mitano ijayo ,baada ya kuzindua mpango huo jana katika mkutano  maalum wa kazi.(Picha na Mwamvua Mwinyi)

Na Mwamvua Mwinyi, Pwani

MKUU wa mkoa wa Pwani mhandisi Evarist Ndikilo amezindua mpango mkakati wa kudhibiti ukimwi wa miaka mitano ijayo lengo likiwa kupambana na maambukizi mapya ya gonjwa hilo.
Amesema mkoa huo ni miongoni wa mikoa  kumi nchini iliyo na kiwango cha maambukizi ya virusi  vya ukimwi juu ambapo una kiwango cha asilimia 5.9 wakati kitaifa ni 5.1.
Mhandisi Ndikilo aliyasema hayo ,katika mkutano  maalum wa kazi ambao agenda juu ilikuwa  ni kuzindua mpango huo ,uliofanyika  ukumbi wa mikutano uliopo ofisi  ya mkuu wa mkoa wa Pwani,Kibaha.
Alielezea kuwa taarifa ya matokeo ya tathmini ya maambukizi ya VVU kitaifa iliyofanyika mwaka 2011/2012 mkoa huo ulikadiriwa kuwa na kiwango cha maambukizi ya VVU kwa kiasi hicho ambacho ni kikubwa.
Mhandisi Ndikilo alisema kwa kuanza na mpango mkakati huo utasaidia kupunguza kiwango cha maambukizi ya virusi hivyo mkoani hapo.
“Huu ni mwitiko wa agizo alilolitoa rais  mstaafu wa awamu ya nne  Jakaya Kikwete alipozindua taarifa ya matokeo ya utafiti wa viashiria vya VVU na ukimwi na malaria THMIS mwaka 2011/2012”
 
Mhandisi Ndikilo alisema Kikwete aliagiza kila mkoa uandae mpango mkakati wa kudhibiti ugonjwa huo hatari ambao utalenga kudhibiti vichocheo vya maambukizi kulingana na eneo husika.
Alitaka mkakati ufanyiwe kazi na utekelezaji kwa vitendo pasipo kuuweka kwenye makabati na kuishia kwenye makabrasha.
Aidha mhandisi Ndikilo aliwaomba viongozi wa dini mkoani humo  kushirikiana na serikali kuhubiri kwa waumini kuwa na maadili mema na kuachana na ngono zembe.
“Mapadre na mashehe nyie pia ni msaada mkubwa  kusaidia hili  ,nawaomba tushirikiane kwa hili  licha ya vitabu vya dini kutokubaliana na masuala haya hasa  ya kuhubiri matumizi ya kondom  ” alisema mhandisi Ndikilo.
Mkuu huyo wa mkoa alitoa ushauri wa kutumiwa kwa vikundi vya sanaa  na maigizo ili kufikisha ujumbe wa jamii kupitia sanaa.
Alikemea  vigodoro na mikesha isiyo na tija  ambayo baadhi ya watu huitumia vibaya na kusababisha kuugua magonjwa ya zinaa na ukimwi.
Mratibu wa ukimwi mkoani Pwani Grace Tete alieleza kuwa watahakikisha wanatekeleza mpango huo pasipo kuishia kwenye makabati.
Grace alisema mpango huo utekelezaji wake ni hadi ifikapo 2020 na unalengo la  kufikia sifuri 3 ambazo ni maambukizi mapya,ya unyanyapaa na sifuri ya vifo  vitokanavyo na ukimwi kutoka kwa mama kwenda kwa mtoto.
Alisema mpango mkakati utatumiwa na halmashauri zote za mkoa kuanzia sasa ili kukabiliana na janga la  gonjwa hilo.
Nae msaidizi wa shehe  mkuu na kadhi wa mkoani hapa ,Hamis Mtupa aliwaasa wanandoa waache michepuko na badala yake wawe waaminifu kwenye ndoa zao ili kujiepusha na magonjwa ya zinaa.
Mtupa alisema kuhusu agizo la  mkuu wa mkoa wamelipokea hivyo ametoa wito kwa viongozi wengine wa dini kutenga sehemu ya kutoka elimu juu ya ukimwi.

No comments:

Post a Comment