Thursday 31 August 2017

Shirika la Posta Tanzania limekusanya madeni ya shilingi bilioni 7.6.

1.JPEG
Mwenyekiti wa Kamati ya Bunge ya Miundombinu Mhe. Prof. Norman Sigala King (katikati), akiongoza kikao cha Kamati yake na Shirika la Posta Tanzania (TPC), kilichofanyika mjini Dodoma. Kulia ni Naibu Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano Eng. Edwin Ngonyani na kushoto ni Makamu Mwenyekiti wa Kamati hiyo Mhe. Moshi S. Kakoso.
2.JPEG
Naibu Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano Eng.  Edwin Ngonyani, akifafanua jambo kwa  Kamati ya Bunge ya Miundombinu  katika kikao chao na Shirika la Posta Tanzania (TPC), kilichofanyika mjini Dodoma. Kulia ni Mwenyekiti wa Kamati hiyo Mhe. Prof. Norman Sigala King na kushoto ni Naibu Katibu Mkuu wa Wizara hiyo, Sekta ya Mawasiliano Eng. Angelina Madete.
3.JPEG
Mwenyekiti wa Bodi ya Shirika la Posta Tanzania (TPC), Luteni Kanali mstaafu Haruni Kondo, akitoa taarifa ya Shirika hilo kwenye kikao chao na Kamati ya Bunge ya Miundombinu kilichofanyika mjini Dodoma. Kulia kwake ni mjumbe wa Kamati hiyo Mhe. Anna Lupembe.
4.JPEG
Mjumbe wa Kamati ya Bunge ya Miundombinu Mhe. Anna Lupembe (wa kwanza kulia), akichangia hoja katika kikao cha Kamati hiyo na Shirika la Posta Tanzania (TPC), kilichofanyika mjini Dodoma. Kushoto kwake anayesikiliza ni Mwenyekiti wa Bodi ya Shirika hilo Luteni Kanali mstaafu Haruni Kondo.

Shirika la Posta Tanzania (TPC), limefanikiwa kukusanya madeni ya muda mrefu kutoka kwa taasisi za Serikali, mashirika ya umma na sekta binafsi kiasi cha shilingi bilioni 7.6.
Hayo yameelezwa na Naibu Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano Eng. Edwin Ngonyani katika kikao cha Kamati ya Bunge ya Kudumu ya Miundombinu kuhusu utekelezaji wa majukumu ya Shirika hilo kilichofanyika mjini Dodoma ambapo amesema makusanyo hayo ni kati ya jumla ya shilingi bilioni 12 ambazo Shirika hilo linadai wateja wake kuanzia mwaka 2011 hadi mwezi Juni mwaka huu.
“Hakikisheni mnamalizia makusanyo ya deni lililobaki, kwani Shirika linahitaji kuendelea na kupata faida kupitia makusanyo haya”, amesema Naibu Waziri Ngonyani.
Naye Mwenyekiti wa Kamati ya Bunge ya Kudumu ya Miundombinu Mhe. Prof. Norman Sigala King ameiomba Serikali kuliondoa Shirika hilo kwenye orodha ya mashirika yanayotaka kubinafsishwa.
Ameongeza kuwa Serikali ikitekeleza jambo hilo, italiwezesha Shirika hilo kujiendesha kibiashara, kuzalisha faida na kukabiliana na changamoto za ushindani kwenye soko.
Aidha, amelitaka Shirika hilo kuwa wabunifu katika utoaji wa huduma zake kwa wananchi kwa kutumia Teknolojia za kisasa zaidi badala ya kutumia mifumo ya kizamani.  
Kwa upande wake Mwenyekiti wa Bodi wa Shirika hilo Luteni Kanali mstaafu Bw. Haruni Kondo, ameiomba Kamati hiyo kuendelea kushirikiana na Shirika hilo na kulisaidia ili liweze kutoa huduma kwa wananchi kwa wakati na kwa ufanisi.
Taasisi za Serikali na Mashirika ya Umma yanaendelea na utekelezaji wa agizo la Rais wa Awamu ya Tano wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. John Pombe Magufuli ya kuhakikisha kuwa yanajiendesha kwa faida, kuongeza ukusanyaji wa mapato na kudai madeni ya muda mrefu ili fedha hizo ziweze kutumika kuwahudumia wananchi katika nyanja mbalimbali kama vile za elimu, afya na ujenzi wa miundombinu.
 
Imetolewa na Kitengo cha Mawasiliano Serikalini, Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano

No comments:

Post a Comment