Tuesday 29 August 2017

Mbivu na mbichi za Coutinho ndani ya masaa 48



Yamebaki masaa yasiyozidi 48 kwa dirisha la usajili kufungwa,Coutinho bado hakijaeleweka. Barcelona jana wamethibitisha kwamba wanahitaji mchezaji mwingine huku Liverpool wakikaza kwamba Coutinho hauzwi.
Coutinho yuko nje kwa majeraha na hajawahi kuonekana uwanjani tangia ligi ianze. Rafiki wa daktari wa klabu ya Liverpool ambaye pia ni daktari aitwaye Simoni ameeleza kwamba majeraha ya Coutinho yamechangiwa na msongo wa mawazo unaomuandama kiungo huyo.
“Majeraha ya Coutinho? Yameletwa na msongo wa mawazo lakini kwa sasa yuko vizuri, lakini mambo yanayoendelea sasa kuhusu soka lake yamekuwa yakimsumbua sana kiakili na hii imempa mawazo, Coutinho ni rafiki yangu na mimi najua mengi kuhusu majeraha yake” alisema Simoni.
Simoni amesema amekutana na Coutinho na wameongea mengi ikiwemo uwezekano wake kuhamia Barcelona lakini hakuweka wazi kuhusu nini amesema kiungo huyo kuhusu tetesi za kuhamia katika klabu ya Barcelona. Coutinho yupo katika kikosi cha Brazil kinachojiandaa kucheza na Ecuador wiki hii.
Wakati huohuo mkurugenzi wa masuala ya ufundi wa Barcelona  Robert Fernandez ameonesha kwamba bado Barca wanamtaka Coutinho baada ya kusema kwamba klabu yao bado ina nafasi kwa mchezaji mmoja mkubwa ndani ya klabu hiyo.

“Kuna mchezaji tunaongea naye na anaweza kutua katika klabu yetu, maongezi bado yanaendelea na tuna matumaini tutaishia pazuri, mchezaji mmoja anaweza kutua au hata wawili ila tuna matumaini makubwa ya usajili” alisema Robert Fernandez.

No comments:

Post a Comment