Thursday 20 July 2017

Uganda wanabadili Katiba

Serikali ya Uganda inafanya juhudi za kubadilisha Katiba ya nchi hiyo na kuondoa kipengele kinachoweka ukomo wa umri wa mtu kuwania urais na hivyo kumuandalia mazingira Rais Yoweri  Museveni aendelee kuitawala nchi hiyo.
Akizungumzia suala hilo mjini Kampala Mshauri wa Rais, David Mafabi amesema  kuwa kuna juhudi zinafanyika ili kuondoa kipengele hicho na hivyo kumfanya Rais Museveni awanie tena kiti cha urais katika uchaguzi ujao.
Hilo ni jaribio jingine la kumfanya Rais Museveni aendelee kuitawala Uganda baada ya mwaka 2005 kufanyika marekebisho ya Katiba yaliyoondoa kifungu kinachoweka ukomo wa rais kuongoza kwa mihula miwili.
Katiba ya Uganda inaeleza kuwa, mtu haruhusiwi kuwania urais akiwa na miaka 75, lakini pia inaeleza kuwa umri wa anayetaka kuwania urais ni lazima uwe 35 na kuendelea.
Wabunge wa chama tawala nchini Uganda cha NRM wanaounga mkono marekebisho hayo wanadai kuwa, sheria hiyo ya ukomo wa umri ikiendelea kuwepo itakuwa kikwazo kwa raia wa nchi hiyo wenye umri mkubwa lakini wenye uwezo wa kuendelea kuongoza nchi hiyo.
Mpango huo unaonekana wazi kuwa, unalenga kumuandalia mazingira Rais Museveni kuwania tena urais mwaka 2021, atakapokuwa na umri wa miaka 76 ameitawala nchi hiyo  tangu mwaka 1986.

Tayari vyama vya upinzani nchini Uganda vimetangaza kuupinga mpango huo. Kizza Besigye, kiongozi mkongwe wa upinzani nchini uganda amewata wananchi wa nchi hiyo kuyakataa marekebisho hayo ya katiba.

No comments:

Post a Comment