Friday 29 September 2017

Manchester City yapata pigo kwa Aguero

MSAMBULIAJI wa Klabu ya Soka ya Manchester City na timu ya taifa ya Argentina, Sergio Kun Aguero, amepata ajali ya gari usiku wa jana akiwa njiani kuelekea uwanja wa ndege nchini Uholanzi ambako alikuwa amehudhuria tamasha la muziki. 
Kwa mujibu wa ripoti, Aguero, 29, amevunjika mbavu na atakuwa nje ya uwanja kwa takribani miezi miwili na atakosa mchezo dhidi ya mabingwa watetezi wa ligi kuu nchini England klabu ya soka ya Chelsea utakaopigwa Jumamosi hii.
Picha zilizosambaa katika baadhi ya mitandao kutoka nchini Uholanzi zimeonyesha gari ndogo ambayo Aguero alikuwepo na dereva wake ikiwa imegonga nguzo katikati ya jiji la Amstedam huku ikiripotiwa kuwa hakuna aliyepoteza maisha zaidi ya kuumia.
Awali aliweka picha kwenye ukurasa wake wa mtandao wa kijamii wa Instagram ikimuonyesha yeye na msanii kutoka Uholanzi anayefahamika kwa jina la Maluma ambaye ndiye aliyemualika staa huyo wa Argentina katika tamasha hilo

No comments:

Post a Comment