Wednesday 20 May 2015

Wanafunzi UDSM wapigwa mabomu wakidai mikopo.

 
Mkurugenzi Msaidizi wa Habari, Elimu na Mawasiliano wa HESLB, Cosmas Mwaisobwa.
 
Jeshi  la Polisi Mkoa wa Kinondoni, limetumia mabomu ya machozi kuwatawanya  Wanafunzi wa Chuo Kikuu Cha Dar es Salaam (UDSM), wanaoishi katika hosteli za Mabibo ambao walikuwa wakiandamana kudai fedha zao za kujikimu.
Walichukua hatua hiyo kutokana na kucheleweshewa  mikopo na Bodi ya Mikopo ya Wanafunzi wa Elimu ya juu (HELSB).
Tukio hilo lilitokea usiku walipoandamana kudai wawekewe fedha kwenye akaunti zao ambazo zimecheleweshwa kwa wiki 11. 
 
Wanafunzi hao waliondoka Mabibo saa 4:00 usiku kwa maandamano kuelekea UDSM ili kuwashirikisha wenzao kushinikiza uongozi kufatilia madai yao ndipo walipokutana na Polisi waliolazimika kutumia mabomu ya machozi kuwatawanya baada ya kushindwa kutii amri ya kusitisha maandamano.
 
Katika purukushani hizo zilizodumu dumu kwa saa tatu, Polisi walitumia mabomu mengi kuwatawanya wanafunzi hao huku  wanafunzi watatu wakikamatwa na wengine watatu wakijeruhiwa.
 
Licha ya kudhibitiwa na Jeshi hilo, jana wanafunzi hao waliendelea na mgomo wa kutoingia darasani mpaka watakapolipwa fedha zao.
 
Rais wa Serikali ya wanafunzi (Daruso) Irene Ishengoma, alisema maandamano hayo yalitokea baada ya wanafunzi kutangaziwa kuwa watakopeshwa Sh. 20,000 na chuo kwa ajili ya kujikimu wakati wakisubiria malipo yao.
 
 “Baada ya kusubiria kwa muda mrefu, uongozi wa chuo ulituahidi kutukopesha Sh. 20,000 kwa wanafunzi 7,000 ambao wanaidai HESLB tangu Mei 8, mwaka huu, walipaswa kutuwekea fedha zetu,” alisema.
 
Alisema baada ya tamko hilo kutoka Serikali ya wanafunzi,  wanafunzi hao waligoma kupokea fedha hizo kwani  kiwango hicho ni kidogo.
 
Ishengoma alisema  baada ya mvutano huo walikubaliana kutoingia darasani mpaka watakapolipwa madai yao.
 
Aliongeza kuwa walipozungumza na uongozi wa chuo waliahidiwa kuwa fedha hizo zitawekwa leo, hivyo walejee madarasani.
Alisema wanafunzi hawakukubaliana na taarifa hizo kwani wao waliachokuwa wakitaka ni HESLB kuwalipa fedha zao.
 
“Kwanini tulipwe Sh. 20,000 wakati tunaidai bodi Sh. 450,000?” Hii haikubaliki kwani hivi sasa maisha yamepanda na wanafunzi wengi wanaishi kuwa kukopa,” alisema.
 
Makamu Mkuu wa Chuo hicho, Prof. Rwekaza  Mukandala, alisema amekutana na uongozi wa Daruso kujadiliana namna ya kutatua tatizo hilo.
 
Alisema wamekubaliana kuwa wanafunzi wote wangelipwa fedha zao zote jana kwani fedha hizo zimeshafika HESLB.
Alisema walilazimika kuwakopesha Sh. 20,000 wakiamini fedha zao zitalipwa ndani ya muda mrefu.
 
“Leo (jana) fedha zitawekwa katika akaunti za wanafunzi ambazo walikuwa wakidai,” alisema.
 
Aliongeza kuwa bado chuo kinafanya tathmini ya uharibifu uliotokea wakati wa maandamano ya wanafunzi hao kwani inasemekana walivunja milango, madirisha na kupasua baadhi ya vioo vya magari.
 
“Kuna taarifa kuwa kuna wanafunzi watatu ambao waliumia katika tukio hilo, lakini hivi sasa wanaendelea vizuri baada ya kupatiwa matibabu na kuruhusiwa,” alisema. 
 
Mkurugenzi Msaidizi wa Habari, Elimu na Mawasiliano wa HESLB, Cosmas Mwaisobwa, alisema wanajitahidi kushughulikia madai ya wanafunzi wa vyuo vyote ambavyo vinanufaika na fedha za Bodi hiyo.
 
“Hatuwezi kusema ni lini au saa ngapi tutakuwa tumewaingizia fedha hizo kwani hatulipi kwa chuo kimoja bali ni vyuo vyote ambavyo vinanufaika na HESLB,” alisema.

No comments:

Post a Comment