Saturday 23 May 2015

Kamati Kuu yasema akina Lowassa huru

  Lowassa: Ni safari ya matumaini
  Makamba: Safari ya ushindi imeanza
Mwenyekiti wa CCM Taifa, Rais Jakaya Kikwete na Katibu Mkuu wa CCM, Abdulrahman Kinana, wakiwa kwenye kikao cha Kamati Kuu.
Hatimaye Kamati Kuu ya Chama cha Mapinduzi (CCM) imewafutia adhabu makada sita wa chama hicho kwa kuanza kampeni za urais mapema kinyume na kanuni na taratibu za chama.
 
Waliofutiwa adhabu ni mawaziri wakuu wastaafu, Edward Lowassa na Frederick Sumaye, Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa, Bernard Membe, Waziri wa Kilimo, Chakula na Ushirika, Stephen Wassira, Naibu Waziri wa Mawasiliano, Sayansi na Teknolojia, January Makamba na Mbunge wa Sengerema, William Ngeleja.
Katibu wa Itikadi na Uenezi wa CCM, Nape Nnauye, aliwaambia waandishi wa habari jana, mara baada ya kikao hicho kumalizika na kufikia uamuzi huo.
"Adhabu  hiyo kwa sasa imemalizika na wanachama hao wameruhusiwa kuendelea na shughuli zao katika chama," alisema Nape. 
 
Hata hivyo, CC imewataka wanachama hao na watu wengine wenye nia ya kugombea urais kupitia CCM kuzisoma, kuziheshimu na kuzizingatia kanuni za maadili ya chama  na kanuni zingine zinazoongoza mchakato huo ili wasikumbwe na adhabu ya kuzivunja kanuni hizo.
 
Alisema Kamati Kuu ilipokea na kutafakari taarifa ya Kamati ya Usalama na Maadili ambayo ilipitia adhabu waliyopewa wanachama hao waliokiuka kanuni za maadili iliyodumu kwa kipindi kisichopungua miezi 12 na kupewa onyo kali.
 
Adhabu yao ilianza tangu Februari 18, mwaka jana na ilitarajiwa kumalizika Februa 18, mwaka huu.  Hata hivyo,  Februari 28, mwaka huu Kamati hiyo ilikutana na kusema adhabu bado inaendelea.
 
Maamuzi ya kamati hiyo, yamekuja baada ya kutafakari taarifa ya Kamati ya Maadili iliyokutana mapema jana. 
 
KIKAO CHA DHARURA
 
Kabla ya maamuzi ya Kamati Kuu, kilifanyika kikao cha dharura ambacho kiliwahusisha vigogo wa juu wa chama hicho, hatua iliyofanya kikao cha CCM kuahirishwa hadi jioni jana.
 
Taarifa zilizozifikia gazeti hili zilieleza kuwa kikao hicho kilihudhuriwa na Mwenyekiti, Rais Kikwete, Katibu Mkuu, Abdulahaman Kinana, Makamu Mwenyekiti Bara, Phillip Mangula na Makamu Mwenyekiti, Zanzibar, Dk. Ali Mohamed Shein,
Chanzo chetu cha habari kilifahamisha kuwa Mwenyekiti, alikuwa anasisitiza kufutwa kwa adhabu hiyo ili wapate nafasi ya kugombea, huku mjumbe mwingine aking’ang’ania isifutwe.
 
Hata hivyo, Nape alipoulizwa kuhusiana na kikao hicho alisema hakukuwa na kikao chochote zaidi ya cha maadili kilichofanyika na wajumbe kutawanyika.
Aidha, alisema wale wote wanaotaka kugombea, yaani waliokuwa kwenye adhabu na wengine watakojiingiza katika kampeni mapema na kukiuka miiko na maadili ya chama, taarifa za kukiukwa kwao zitatumika kwenye mchujo wa nafasi walizoziomba hasa kwenye urais.
 
"Taarifa hizo zitapima na kuangalia kwa sifa, nafasi walizoziomba kama wanafaa au hawafai katika kupata uteuzi wa nafasi wanayoiomba, sehemu hii ni ya muhimu sana," alisema.
 
Hata hivyo, alisema watu wanaangalia vikao hivyo vya CCM na wana presha za makambi hivyo vitu vinavyoenea kwenye mtandao na mtaani ni vya uongo kwani Kamati Kuu haijatoa onyo kali kwa wanachama hao.
 
"Hakuna barua wala onyo kali zaidi ya haya niliyozungumza,"alisema.
Awali akitoa taarifa kwa mwenyekiti wa chama hicho, Rais Jakaya Kikwete, Katibu Mkuu wa CCM, Abdurahaman Kinana, alisema wajumbe waliohudhuria ni 30 kati ya 32  waliotakiwa kuwepo.
Wajumbe ambao hawakuwepo ni Makamu wa Rais, Mohammed Gharib Bilal ambaye yupo China.
 
LOWASSA
Kufuatia maamuzi hayo Lowassa alisema uadilifu wake ndani ya chama umemfanya afutiwe adhabu hiyo na kwamba yaliyotokea ni sehemu ya safari yake ya matumaini.
Akiongea kwa niaba ya Waziri Mkuu aliyejiuzulu na Mbunge wa Monduli,  Msemaji wake, Aboubakar Liongo, alisema  “Lowassa anaendelea na vikao na yaliyojitokeza kuhusiana na adhabu aliyopewa ni sehemu ya safari ya matumaini,” alisema.
Aidha, alisema  Lowassa  anajiandaa kutangaza nia wiki ijayo, jijini Arusha.
 
MAKAMBA
Kwa upande wake , Makamba alisema amefurahia kufutiwa adhabu hiyo na sasa safari ya ushindi  inaanza.
 
SUMAYE
Alisema walikuwa na adhabu ya mwaka mmoja na iliisha mwezi Februari, walichokuwa wanasubiri ni vikao vya maamuzi kuketi.
Alisema sasa wako huru na watatekeleza matakwa ya chama katika kugombea uchaguzi mkuu.
 
MEMBE 
Alipopigiwa simu kuzungumzia kufutiwa adhabu hiyo alijibu kwa kifupi “No comment” (sina cha kuzungumza)

No comments:

Post a Comment