Saturday 23 May 2015

Hatimaye walemavu Mchikichini warejea kwenye vibanda vyao


Siku moja baada ya wafanyabiashara wenye ulemavu wa soko la Mchikichini jijini Dar es Salaam kufunga barabara baada ya kubomolewa meza za biashara zao, serikali imewaruhusu kuendelea na kazi eneo hilo huku ikifanya tathmini ya hasara iliyopatikana.
 
NIPASHE Jumamosi ilishuhudia jana meza za wafanyabiashara hao zilizovunjwa usiku wa kuamkia juzi zikijengwa upya.
 
Wafanyabiashara hao juzi walilazimika kufunga barabara ya Kawawa na Uhuru kwa saa sita baada ya kukuta meza zao za biashara zikiwa zimevunjwa.
 
Akizungumza na gazeti hili jana, mmoja wa wafanyabiashara hao ambaye anayejihusisha na uuzaji wa mabegi sokoni hapo, Mfaume Seleman, alisema kuwa viongozi wao walipokea barua kutoka kwa Mkurugenzi wa Manispaa ya Ilala.
Alisema barua hiyo imewataka waendelee kufanya shughuli zao katika maeneo waliyotoka au walipokuwa wakifanya biashara zao.
 
Alisema barua hiyo imeeleza kuwa, Serikali imeliona tatizo hilo na kulifanyia kazi kwa kufanya uchunguzi kwa kushirikiana na uongozi wa wafanyabiashara hao.
 
Seleman alisema kuanzia jana viongozi wao wameanza kukutana na serikali kufanya vikao ili kupata ufumbuzi wa kudumu.
Barua hiyo ambayo NIPASHE imeona inaeleza kuwa, uchunguzi unafanyika na itakapobainika nini kilijiri kwa waathirika Halmashauri ya Ilala itakaa na waathirika ili kuweza kubaini hasara walizopata na fidia

No comments:

Post a Comment