Jeshi la Polisi mkoa wa
Mbeya limeendelea kufanya misako, operesheni na doria zenye tija katika
maeneo mbalimbali ili kudhibiti uhalifu na wahalifu na limekuwa
likishirikiana na wananchi na wadau wengine katika jitihada hizo za
kukabiliana na uhalifu na wahalifu na kupata mafanikio makubwa ikiwa ni
pamoja na kupungua kwa matukio makubwa ya uhalifu. Mafanikio
yaliyopatikana katika Misako ni kama ifuatavyo:-
KUPATIKANA KWA SILAHA ZA KIVITA.
Mnamo tarehe 04.09.2016 majira ya
saa 23:45 usiku huko katika kitongoji cha Sinza, Wilaya ya Chunya karibu
na ofisi ya Usalama wa Taifa askari Polisi wakiwa Doria waliwatilia
mashaka watu wawili waliokuwa kwenye pikipiki isiyotambulika na kisha
kuwafyatulia risasi na ndipo watu hao waliporusha mfuko ambao baada ya
kupekuliwa uliokutwa na silaha moja aina ya Smg ambayo imefutwa namba
zake, magazine mbili, bomu moja la kurusha kwa mkono na Risasi 24.
Watu hao wanaodhaniwa kuwa ni
majambazi walikimbia na pikipiki na inadhaniwa kuwa mmoja kati yao
amepigwa risasi. Kamanda wa Polisi Mkoa wa Mbeya Naibu Kamishna wa
Polisi DHAHIRI A. KIDAVASHARI anatoa wito kwa wananchi kwamba pale
watakapoona mtu mwenye majeraha anayetibiwa bila kufuata utaratibu watoe
taarifa.
KUPATIKANA NA NOTI BANDIA.
Katika msako uliofanyika mnamo
tarehe 04.09.2016 majira ya saa 19:00 jioni huko Maeneo ya Mwanjelwa
jijini, Mtu mmoja mkazi wa Nonde aliyefahamika kwa jina la JOSEPH SAUDEN
(34) alikamatwa akiwa na noti bandia tatu za elfu tano zenye namba PP 1547999, GG 2937838 na BY 1547949 ambazo ni bandia zote zikiwa na thamani ya Tsh.15,000/=.
Mtuhumiwa alikamatwa akiwa anataka
kununua nguo kwenye duka la Bwana NOVATUS KAVISHENI. Mtuhumiwa
amekamatwa na upelelezi unaendelea.
Aidha Jeshi la Polisi Mkoa wa
Mbeya limeendelea kukabiliana na matukio makubwa ya uhalifu pamoja na
wahalifu. Jitihada zinaendelea kwa kushirikiana na wananchi kuhakikisha
Mkoa wetu unakuwa mahala salama. Kumekuwa na matukio 01 ya mauaji kama
ifuatavyo:-
MAUAJI.
- Mnamo tarehe 04.09.2016 majira ya saa 00:15 usiku huko katika kijiji cha Iduya Wilaya ya Mbarali, Mzee wa miaka 74 Mkazi wa Iduya aitwaye JACOB NGOLELA aliuawa kwa kukatwa shoka kichwani na shingoni.
Marehemu alikuwa na wake watatu na
siku ya tukio alikuwa amelala nyumbani kwa mke mdogo aitwaye ELIZABETH
KAMILO (62) mkazi wa Iduya.
Mbinu iliyotumika na watu hao
ambao idadi yao haikufahamika waliokuwa wamefunika nyuso zao kwa kofia
za mizula ni kuondoa matofali yaliyowekwa dirishani na
kuingia ndani kisha kumkata shoka marehemu akiwa kitandani
na kumuamuru mke wake asipige kelele. Chanzo cha mauaji hayo ni
mgogoro wa muda mrefu wa kugombea mashamba baina ya marehemu
na mtoto wake aitwae MUSA JACOB NGOLELA (42) mkazi wa Iduya
ambaye amekamatwa. Upelelezi unaendelea.
Jeshi la Polisi Mkoa wa Mbeya pia
linaongeza jitihada za kuzuia na kupunguza ajali za barabarani kwa
kuhakikisha madereva na watumiaji wengine wa barabara wanatii sheria za
usalama barabarani. Aidha kumekuwa na matukio 02 ya ajali za vifo kama
ifuatavyo:-
AJALI ZA VIFO.
- Mnamo tarehe 04.09.2016 majira ya saa 18:45 jioni huko katumba Wilaya ya Rungwe katika barabara kuu ya Tukuyu – Mbeya, Pikipiki isiyofahamika iliyotoroshwa baada ya ajali ikiendeshwa na AMANI LAWRENCE @ Mwangomwango (18) Dereva bodaboda, Mkazi wa Katumba iliacha njia na kupinduka na kusababisha kifo cha dereva huyo na majeruhi kwa AMED MWASAMBOMA (20) Mkazi wa Katumba ambaye alikuwa abiria wa pikipiki hiyo.
Mwili wa marehemu umehifadhiwa
hospitali ya Wilaya ya Rungwe na majeruhi amelazwa hospitalini hapo.
Chanzo cha ajali ni mwendo kasi wa dereva huyo.
- Mnamo tarehe 04.09.2016 majira ya saa 12:15 mchana katika Hospitali ya Rufaa Mbeya, iliyopo Jijini Mbeya, Mtu mmoja aliyefahamika kwa jina la AHABU KIMATILE (28) mkazi wa Mapogolo alifariki dunia wakati akiendelea kupatiwa matibabu hospitalini hapo.
Awali mnamo tarehe 03.09.2016
majira ya saa 14:05 mchana huko kijiji na kata ya Mapogolo, Wilaya ya
Mbarali katika barabara ya Madibira kwenda Rujewa, marehemu akiendesha
pikipiki yenye namba za usajili T.416 BHT aina ya Sanlg iligongana na
pikipiki nyingine yenye namba za usajili T.372 ABY aina ya Honda
iliyokuwa ikiendeshwa na ZAKI YUSUPH (30) mkazi wa Rujewa na kusababisha
majeruhi kwa waendesha Pikipiki hao na kulazwa hospitali ya Wilaya ya
Mbarali kabla ya marehemu kuhamishiwa Rufaa Mbeya.
Chanzo cha ajali ni uzembe na mwendo kasi kwa waendesha pikipiki hao.
WITO:
Kamanda wa Polisi Mkoa wa Mbeya
Naibu Kamishna wa Polisi DHAHIRI A. KIDAVASHARI anatoa wito kwa jamii
kuacha tabia ya kutaka kupata mali au utajiri kwa njia ya mkato na
badala yake wafanye kazi halali ili wapate kipato halali. Pia
anasisitiza kuwa maendeleo hayapatikani kwa kufanya kazi hama biashara
haramu, watumie fursa zilizopo Mkoa wa Mbeya kujitafutia ajira. Aidha
anaendelea kutoa wito kwa madereva na watumiaji wa barabara kuwa makini
hasa kwa kufuata na kuzingatia sheria na alama za usalama barabarani ili
kuepuka ajali zinazoepukika.
Imesainiwa na:
[DHAHIRI A. KIDAVASHARI – DCP]
KAMANDA WA POLISI MKOA WA MBEYA.
No comments:
Post a Comment