Friday 25 March 2016

Zaidi ya Watu 150 Wamejitokeza kuhakiki Silaha Zao


diwani_athumaniNa. Kalonga Kasati
Mkurugenzi  wa Upelelezi wa Makosa ya Jinai, Kamishna wa Polisi Diwani Athumani amesema hadi kufikia sasa zaidi ya watu 150  wamejitokeza  kuhakiki wa  silaha zao, katika hatua ya  kutii agizo la Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Paul  Makonda.

“Baada ya Mheshimiwa Rais John Pombe  Magufuli  kufanya uhakiki wa silaha zake  hivi karibuni, watu Zaidi ya 150 Wakiwemo viongozi mbalimbali waliopo Serikalini, Viongozi wastaafu, Mabalozi wa nchi Mbalimbali, Wafanyabiashara na  wabunge wamejitokeza  kuhakiki  silaha zao, na wengine wameonesha nia ya kufanya hivyo,  Hata hivyo tusingependa kutaja majina yao kwa sababu za kiusalama” amesema Kamishna wa Polisi Athumani

Athumani amesema kuwa, lengo la kufanya uhakiki wa silaha ni pamoja na kuboresha hali ya usalama na kuwajua Watumiaji, kuwatambua tena wamiliki wa silaha pamoja na kuwa wanawatambua isipokuwa  zinaweza kutokea Sababu mbalimbali zitakazofanya wasiendelee kumiliki silaha hizo ikiwemo vifo na ulemavu na  kusema kuwa  Wangependa kufahamu taarifa za namna hiyo, ameongeza kuwa  zoezi hili sasa ni la nchi nzima si kwa Mkoa wa Dar es Salaam pekee kama ilivyokuwa hapo awali.

Aidha, wakazi wa  mkoa wa Dar es Salaam wanaweza  kuhakiki silaha zao katika vituo vya  Osterbay Polisi, Temeke Chang’ombe Polisi na Ilala central Polisi, ambapo wanatakiwa kwenda na  kitabu(firearm  licence book), Picha ndogo nne za mhusika,  pamoja na  anwani sahihi ya mahali anapoishi mhusika.

Vilevile, amewataka viongozi mbalimbali na wananchi wanaomiliki silaha kujitokeza kwa ajili ya kufanya uhakiki wa Silaha zao huku akisisitiza kwa wakazi wa Mkoa wa Dar es salaam, wanaweza kuonana na Kamanda wa Polisi wa Kanda Maalum ya Dar es salaam, Simon Sirro na kwa wakazi wa Mikoani waonanae na makamanda wa polisi wa Mikoa yao kwa ajili ya kupewa msaada na maelekezo zaidi ya taratibu  za kufuata ili waweze kufanya uhakiki wa  silaha zao.

No comments:

Post a Comment