Sunday 12 April 2015

Chadema kutumia chopa tano kutetea majimbo


Arusha/Mtwara. Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), kimetangaza mkakati wake katika Uchaguzi Mkuu kwa Mkoa wa Arusha, lengo likiwa ni kuzoa majimbo na kata zote.
Mwenyekiti wa madiwani wa chama hicho mkoani Arusha, Isaya Doita alisema jana kuwa: “Tunakusudia kutumia chopa tano Kanda ya Kaskazini, magari ya kisasa ya kampeni yenye uwezo wa kuendesha mikutano mikubwa ya hadhara mwaka huu.”
Alisema Chadema Kanda ya Kaskazini kwa kushirikiana na Umoja wa Katiba ya Wananchi (Ukawa), wamejipanga kushinda majimbo yote 33 na kata 673 ya Arusha, Kilimanjaro, Tanga na Manyara.
Doita alisema katika kuhakikisha ushindi unapatikana wamejipanga kuwakutanisha  wagombea wote wa udiwani na ubunge ili kuweka mikakati ya kampeni hizo.
“Ukombozi una gharama zake, sisi tunaomba tushirikiane kwa kuchangiana ili kuhakikisha Watanzania wanakuwa huru,” alisema Doita.
Katika hatua nyingine, Chadema imeitaka Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC), kuweka wazi tarehe za kuanza uandikishaji wa wapigakura mkoani Mtwara.
Uandikishaji wa wapigakura kwa sasa unaendelea katika miji na vitongoji vya Mkoa wa Njombe.
Naibu Katibu Mkuu wa Chadema Bara, John Mnyika alisema maelekezo ya NEC ni kwamba baada ya Njombe ni Mtwara, lakini haijaweka bayana tarehe, mji wala kitongoji kitakachoanza uandikishaji.
Mnyika aliwataka wananchi wa Mtwara kujitokeza kwa wingi wakati uandikishaji utakapokuwa mkoani humo.
Alisema chama chake kinaazimia kuifanya Lindi na Mtwara kuwa Kanda ya Kusini wakati Ruvuma itakuwa katika Kanda ya Nyanda za Juu Kusini kiutendaji.

No comments:

Post a Comment