Thursday 30 June 2016

Wabunge watatu wa Ukawa wasimamishwa kutohudhuria vikao bungeni

  Na Golden Mwakatobe
 
Bunge limeridhia pendekezo la adhabu ya kumsimamisha vikao 10 kuanzia leo Mbunge wa Mbeya Mjini, Joseph Mbilinyi baada ya kutiwa hatiani na Kamati ya Haki, Maadili na Madaraka ya Bunge kwa kudharau mamlaka ya Spika.
Mwenyekiti wa Kamati hiyo Kepten Mstaafu George Mkuchika alisema alinyoosha kidole cha kati kwenda juu cha mkono wa kulia huku vingine akivikunja  jambo ambalo ni matusi na dharau kwa mamlaka ya Bunge.

Naibu Spika Dk Tulia Ackson amewasimamisha Wabunge wengine wawili wa Ukawa,ambao ni Mbunge wa  Ubungo (Chadema) Saed Kubenea kwa kutohudhuria vikao vitano kuanzia leo baada ya kutiwa hatiani na Kamati ya Haki, Maadili na Madaraka ya Bunge kuwa alisema uongo Bungeni.

Mbunge mwingine  aliyesimamishwa ni  Mbunge wa Simanjiro (Chadema) James Ole Millya kutohudhuria vikao vitano kuanzia leo baada ya kutiwa hatiani na Kamati ya Haki, Maadili na Madaraka ya Bunge kuwa alisema uongo Bungeni.

Waziri Mkuu Kassim Majaliwa ameanza kutoa hotuba ya kuahirisha Bunge na kueleza bajeti ni ya kihistoria tangu nchi ipate uhuru kwa kutenga asilimia 40 ya Sh29.5 trilioni kwa ajili ya miradi ya maendeleo.

No comments:

Post a Comment