Saturday 25 June 2016

Patrick Kahemele ameahidi mambo makubwa

  Na Golden Mwakatobe
 
Patrick Kahemele amesaini mkata wa miaka miwili kuitumikia Simba kama Katibu Mkuu wa klabu hiyo baada ya mabingwa hao wa zamani kukaa kwa muda mfefu bila kuwa na mtendaji mkuu wa shughuli za klabu yao.


Kahemele ameahidi mambo makuu mawili katika uongozi wake wa miaka miwili ndani ya Simba. Jambo la kubwa na kwanza ni kuifanya Simba ijitegemee na kuacha kutegemea mifuko ya watu wachache lakini huu ukiwa ni mpango wa muda mrefu. Jambo la pili ni kuisaidia klabu hiyo kutwaa ubingwa wa ligi kuu ya Vodacom Tanzania bara ilioukosa kwa misimu minne sasa.

“Simba ni timu kubwa, imekuwa na hamu ya mafanikio ndani ya uwanja na nje ya uwanja. Tukizungumza nje ya uwanja, klabu inahitaji kujitegemea na naamini wana Simba wana mawazo mengi, kikubwa ni kukaa na kushirikiana tuweke mawazo yetu pamoja na kuona ni jinsi gani tunaweza tukaikwamua klabu ya Simba kutoka kutegemea mifuko ya watu wachache hadi kuwa klabu inayojitegemea na kusimama yenyewe,” amesema Kahemele ambaye ataanza majukumu yake ya kazi Julai 1 mwaka huu.

“Hiyo ni mipango ya muda mrefu katika kipindi cha miaka miwili ningependa nifanikishe hilo ambalo hata nikiondoka mimi pamoja na viongozi wenzangu tunakuwa tumefanya kitiu flani. Lakini la msingi kabisa ni kuhakikisha msimu ujao lazima ubingwa uende Msimbazi kwasababu Simba ni timu ambayo imezoea kushinda vikombe lakini kazi hiyo inaanzia kwenye usajili, lazima tuwe na timu nzuri, benchi la ufundi zuri, timu ipate kambi na huduma nzuri na vyote hivyo vikiwekwa pamoja hakuna linaloshindikana.”

Anatoa neno kuhusu mashabiki wa ‘mnyama’

“Mashabiki wa Simba ni wastaarabu sana, sijawahi kuona mashabiki wa Simba wakitia presha, mashabiki wa Simba wakikupa shida ujue umewakosea lakini kama hujawakosea hawana shida kabisa.”

No comments:

Post a Comment