Tuesday 27 June 2017

Mchuano wa Urais Nchini Kenya

Rais wa Kenya Uhuru Kenyatta anayewania Urais kwa muhula wa pili, ameiweka wazi ilani ya chama chake cha Jubilee kuelekea Uchaguzi Mkuu utakaofanyika nchini humo August 8, 2017.
Rais Kenyatta ameahidi kuwa serikali yake itaunda nafasi mpya za kazi Milioni 6.5 kwa muda wa miaka mitano atakayokuwa madarakani. Ameeleza kuwa hili litafanyika kwa kuhakikisha kuwa anajenga kiwanda kimoja katika Kaunti zote 47 nchini humo.
Elimu katika Shule za serikali za Sekondari itakuwa bure. Hakuna mwanafunzi yeyote atakayelipa ada ili kupata elimu.
Kenyatta ameahidi kuimarisha sekta ya afya nchini humo kwa kupanua hospitali, kununua vifaa na kuinua kiwango cha tiba katika hospitali za serikali nchini humo Wanawake waja wazito nchini humo wataendelea kujifungua bure na kupata huduma muhimu bila malipo yoyote nchini humo kwa mujibu wa Ilani ya Jubilee.
Kiongozi huyo wa Jubilee ameahidi ikiwa atashinda atajenga makazi ya bei nafuu 500,000 nchi nzima lakini pia mabwawa ya maji 57 kwa lengo la kuimarisha sekta ya kilimo nchini humo.
Pamoja hayo, Kenyatta amesema ikiwa atachaguliwa tena Wakenya wote wataunganishwa na huduma ya umeme kwa muda wa miaka mitatu ya uongozi wake.

Ahadi nyingine iliyotolewa na kiongozi huyu ni kujenga viwanja vipya vya kisasa vya michezo katika maeneo mbalimbali nchini humo.

Mbali na ahadi hizi, rais Kenyatta amesema serikali yake inaimarisha usalama, kujenga reli ya kisasa lakini pia kuinua uchumi wa taifa hilo.

No comments:

Post a Comment