Wednesday 26 October 2016

tamko la serikali kuhusu Takwimu za viashiria vya Ukimwi na Maralia mwaka 2011-2012

1
Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na WatotoMh. Ummy Mwalimu akizungumza na waandishi wa habari wakati alipokuwa akitoa tamko la serikali kuhusu Takwimu za viashiria vya Ukimwi na Maralia mwaka 2011-2012 na kiwango cha maambukizi ya Ukimwi (VVU) kushoto kwake ni Mganga Mkuu wa Serikali Prof. Mohammed Bakari Kambi.

Kwa mujibu wa Takwimu za Viashiria vya UKIMWI na Malaria za mwaka 2011-2012, kiwango cha maambukizi ya Virusi vya UKIMWI (VVU) nchini kinakadiriwa kuwa ni asilimia 5.1 miongoni mwa watu wazima wenye umri kati ya miaka 15 – 49. Takwimu hizi zinaashiria kwamba, kwa kila watanzania 1000, watu 51 miongoni mwao wanaoishi na maambukizi ya VVU. Inakadiriwa kuwa, kuna watu 1,400,000 wanaishi na VVU nchini Tanzania ambapo, watu 839,574 wanapatiwa tiba ya dawa za kupunguza makali ya VVU zinazotolewa katika vituo 4,000 vilikuwa vinatoa huduma hiyo nchi nzima hadi kufikia mwezi Juni mwaka huu (2016).
Serikali ya Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania kupitia Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto kwa kushirikiana na Wadau wake imechukua hatua za makusudi na za haraka katika kukabiliana na Maambukizi ya Virusi vya UKIMWI na UKIMWI. Serikali imefanikiwa kuanzisha na kutekeleza mipango mbalimbali ya kuzuia maambukizi mapya kwa kutoa huduma za kinga, tiba na matunzo kwa walioambukizwa VVU katika ngazi ya vituo vya huduma za afya na ngazi ya jamii. Mikakati yote hii imelenga kuboresha afya kwa kupunguza maambukizi mapya ya VVU na kutokomeza kabisa UKIMWI.  
Mbali na Mipango mikakati na mbinu madhubuti ambazo zimetekelezwa bado takwimu zinaonesha kuwa kiwango cha maambukizi miongoni mwa makundi maalum na yale yaliyo katika hatari zaidi ya kuambukizwa VVU yapo juu kulinganisha na kiwango kilichopo kwa jamii kwa ujumla. 
Kutokana na mazingira yetu makundi maalum ni makundi yaliyo katika hatari zaidi ya kuambukiza na kuambukizwa VVU, kwa kuzingatia takwimu za maambukizi ya VVU kwa makundi haya kuwa juu, Serikali imeainisha makundi haya kama ifuatavyo:- 
Wasichana walio katika umri wa balehe walio katika mazingira hatarishi, vijana walio katika umri wa balehe,  watoto yatima na watoto walio katika mazingira hatarishi (yaani watoto wanaoishi mitaani), wanaume wanaofanya ngono na wanaume wenzao, wanawake wanaofanya ngono kinyume na maumbile, watu wanaotumia dawa za kulevya hasa wale wanaotumia dawa za kulevya kwa njia ya kujidunga sindano, wanawake wanaofanya biashara ya ngono na wateja wao, wafungwa, wakimbizi na wafanyakazi wanao hamahama hasa madereva wa malori ya masafa marefu, wachimba madini na jamii zilizopo katika maeneo ya migodi, wavuvi na jamii zilizopo katika maeneo ya uvuvi, wafanyakazi wa kwenye mashamba makubwa, wajenzi wa barabara  na watu wenye ulemevu.
Kuna ushahidi wa kipiedemilojia kwa programu za VVU na UKIMWI kulenga makundi maalum. Katika nchi zilizo Afrika Kusini mwa Jangwa la Sahara, vijana balehe wenye umri wa miaka 15 hadi 24 wanachangia asilimia 35 ya maambukizi mapya ya VVU. Aidha, kiwango kikubwa cha maambukizi ya VVU nchini Tanzania, kinaonekana miongoni mwa makundi maalum (asilimia 26 miongoni mwa Wanawake wanaofanya Biashara ya Ngono, asilimia 36 miongoni mwa wajidunga na asilimia 25 miongoni mwa wanaume wanaofanya ngono na wanaume wenzao). 
Serikali ya Tanzania kupitia Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto ilianza kutoa huduma za VVU na UKIMWI kwa makundi maalum na yale yaliyo katika hatari zaidi ya kuambukizwa na kuambukiza VVU tangu mwaka 2010 baada ya kufanya tafiti na kugundua kuwa kiwango cha maambukizi ya VVU kiko juu ikilinganishwa na makundi mengine kwenye jamii.  Huduma hizi zimekuwa zinatolewa katika vituo vya kutolea huduma za afya katika ngazi ya Jamii katika Mikoa mbalimbali nchini.
Hivi karibuni kumekuwepo na taarifa kuwa Asasi za Kiraia (za hapa nchini na za Kimataifa) zimekuwa zinapitia katika Afua ya kupambana na UKIMWI ili kuhamasisha mapenzi ya jinsia moja, na hii imepelekea Waziri wa Katiba na Sheria kutamka kupitia vyombo vya habari kuwa atavichukulia hatua za kisheria asasi hizo ambazo zinakiuka taratibu na sheria zilizowekwa na Serikali.
Napenda kutamka kwamba, Wizara yangu halitalifumbia macho suala hili, na napenda kuziasa asasi zote za kiraia za ndani na nje ya nchi kufanya kazi kwa kufuata taratibu na sheria za nchi na kutoa afua zenye lengo la kupambana na maambukizi mapya ya VVU katika makundi haya na jamii kwa ujumla. Aidha nazitaka asasi hizo kutoa huduma bora zenye kiwango cha kimataifa lakini pia huduma zinaoendana na utamaduni, mila na desturi za Mtanzania huku zikizingatia sheria za nchi kama vile sheria ya kanuni ya adhabu, sura ya 16 kama ilivyofanyiwa marakebisho mwaka 2002. 
Tukumbuke kwamba Serikali kupitia Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto ina jukumu la kutoa huduma za Afya na zile za kupambana na UKIMWI bila ubaguzi, na vilevile bila kujali jinsi, kabila, dini, hali ya kifedha, rangi au chama cha mtu yeyote.
Baada ya kubaini changamoto katika utoaji wa huduma za Afya na zile za kupambana na UKIMWI kwa asasi zisizo za Serikali, niliitisha kikao na wadau wa maendeleo wanao fadhili na kutoa huduma za kupambana na UKIMWI katika makundi haya maalum ili niweze kutoa ufafanuzi wa mambo kadhaa ya msingi ikiwemo kuweka bayana suala la kutoa huduma za VVU kwa makundi haya huku tukizingatia taratibu na sheria za nchi (Public Health Approach to HIV programming to PK).
Yafuatayo ni matamko niliyoyatoa na ambayo wote tunapaswa kuyazingatia: 
Serikali itaendelea kutoa huduma za Afya na zile za kupambana na UKIMWI bila ubaguzi wa jinsi, kabila, dini, hali ya kifedha, rangi au chama cha mtu yeyote.
Kwa kuwa maambukizi ya VVU kwa makundi maalum bado yapo juu ukilinganisha na jamii kwa ujumla, Serikali kupitia Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, JInsia, Wazee na Watoto itaendelea kutoa kitita cha huduma kama kitakavyopitiwa na kuainishwa na miongozo ya kutolea huduma za kupambana na UKIMWI katika makundi maalum.
Makundi Maalum kwa mantiki ya Tanzania itabaki kuwa ya kiujumla kama yalivyo tajwa hapo juu ambayo yanaendana na mazingira ya Tanzania, hivyo maana na tafsiri hiyo ifuatwe na kuzingatiwa katika huduma au afua zinazotekelezwa na wadau wote wanao shirikiana na Serikali katika kutoa huduma za VVU na UKIMWI nchini. 
Kila mdau wakati wote atoe huduma kwa mujibu na sheria na kanuni ya adhabu sura ya 16 kama ilivyofanyiwa marekebisho mwaka 2002 inayotaka mtu kuchukuliwa sheria endapo atathibitika kufanya mapenzi na mtu wa jinsia moja., na kama mdau ni shirika lisilo la Serikali pia ana wajibu wa kuzingatia Sheria Na 24 ya Mwaka 2002 ya Asasi zisizo za Kiserikali, na kufuata maadili ya kazi za NGO (NGO code of conduct).
Huduma za Makundi maalum na yale yaliyo katika hatari zaidi ya kuambukizwa na kuambukiza VVU zinazotolewa katika vituo vya kutolea huduma za afya zitaendelea kwa makundi yote isipokuwa huduma za ngazi ya jamii kwa wanaume wanaofanya ngono na wanaume wenzao, hizi zitasubiri mwongozo mpya wa utoaji wa huduma ngazi ya jamii.  Huduma mkoba zinazotolewa na watoa huduma za afya toka vituoni zitaendelea kutolewa kwa mujibu wa miongozo iliyopo. Wizara inaweka msisitizo mkubwa katika kuunganisha huduma zinazofanana na utoaji wa rufaa katika vituo vya huduma za afya kwa mwendelezo wa huduma. Taratibu za utekelezaji zitafafanuliwa na Wizara ndani ya wiki moja.
Kutokana na kuongezeka kwa idadi ya wadau wanaotaka kushirikiana na kuisaidia Serikali katika kutoa huduma hizi, hasa kwa kuzingatia tabia ya kuhama hama kwa makundi haya kutoka eneo moja hadi jingine, kumekuwa na mwingiliano wa huduma zinazotolewa kwa makundi haya, mwingiliao huu unahatarisha ubora wa huduma. Ili kuleta tija, uwajibikaji na uwazi, Mganga Mkuu wa Serikali ataongoza zoezi la kupanga upya wadau katika Mikoa watakayotoa huduma kwa nchi nzima. 
Asasi zote za kiraia za hapa nchini zinazotekeleza afua za VVU na UKIMWI katika Halmashauri lazima ziidhinishwe na Halmashauri husika kabla hazijaruhusiwa kufanya kazi na asasi zisizo za kiserikali za kimataifa. Kwa maneno mengine, Asasi zisizo za kiserikali za kimataifa zitapewa orodha ya asasi za kiraia zilizoidhinishwa kufanya kazi katika Halmashauri au Wilaya husika. Kanuni za Msingi za Ushirikiano (MOU) zitaandaliwa kati ya wadau watatu, yaani Asasi ya Kimataifa, Asasi ya Kiraia ya hapa nchini na Halmashauri au Wilaya husika. Nakala ya Kanuni za Msingi za Ushirikiano (MOU) ziwasilishwe Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto (Idara ya Maendeleo ya Jamii) na Tume ya Taifa ya Kudhibiti UKIMWI. 
Wakati huohuo, mkakati wa usambazaji wa vilainishi hauruhusiwi kutolewa kama afua mojawapo ya kuzuia VVU kwa sasa. Serikali inahitaji muda wa kutosha wa kujiridhisha kuhusu umuhimu wa matumizi yake kama kinga ya kuzuia VVU na pia kuhusu kukubalika katika jamii yetu. Endapo Serikali itaridhia jambo hili, basi hatua stahiki zitachukuliwa ikiwa ni pamoja na kuandaa mipango ya manunuzi na usambazaji wake ikitumia mfumo ya kusambaza vifaa tiba.

No comments:

Post a Comment