Friday 28 October 2016

Duterte: Nimeisikia sauti ya Mungu

 Rais wa Ufilipino Rodrigo Duterte, ameahidi kuacha kutumia lugha ya matusi baada ya kile anachosema kuwa ni kupata ujumbe wa moja kwa moja kutoka kwa Mungu.
Rais huyo, alliyemwita Rais Barack Obama "mwana wa kahaba" na akasema kiongozi huyo anaweza "kwenda jehanamu", amesema amefikia uamuzi huo baada ya kupata ufunuo alipokuwa safarini kutoka Japan.
Amewatusi pia watu wengine mashuhuri. Alimwita kiongozi wa kanisa Katoliki duniani Papa Francis "mwana wa kahaba" (Ufilipino ni taifa lenye Wakatoliki wengi).
Amewahi kumtusi pia waziri wa mambo ya nje wa Marekani John Kerry kwa kumuita "mwendawazimu" na majuzi alimweleza balozi wa Marekani nchini Ufilipino kama "mpenzi wa jinsia moja ambaye ni mwana wa kahaba".
Bw Duterte amesema kuwa alipokuwa kwenye ndege, na watu wengine wote walikuwa wamelala, alisikia sauti ikimuonya: usipokoma, nitaiangusha ndege hii.
Amesema sauti hiyo ilijitambulisha kuwa ilitoka kwa Mungu.
Amewaahidi watu waliokusanyika mji wake wa nyumbani wa Davao kwamba ahadi kwa Mungu ni sawa na ahadi kwa Wafilipino.
Rais Duterte ni kiongozi ambaye msimamo wake na matamshi yake huzua utata mara kwa mara.
Amesomea taaluma ya sheria na alipanda cheo hadi kuwa mwendesha mashtaka kabla ya kuteuliwa kuwa naibu meya wa Davao wakati wa mapinduzi yaliyomuondoa madarakani Ferdinand Marcos mwaka 1986.
Alikuwa meya mwaka 1988 na kushikilia wadhfa huo kwa kipindi cha miaka 10, kabla ya kushinda kiti cha ubunge katika Bunge la Congress halafu akarejea kwenye kiti cha umeya mwaka 2001.
Alijijengea umaarufu kwa kupiga vita baadhi ya matatizo makubwa yanayowakabili Wafilipino - uhalifu, makundi ya uasi, na ufisadi. Yote haya yalipungua kwa kiwango kikubwa wakati alipokuwa kiongozi wa Davao, na kufanya mji huo kuwa mmoja wa miji salama zaidi nchini Ufilipin
o.

Duterte ambaye utawala wake ni wa kipekee kwa kuwa kiongozi mwenye sera za Kijamaa na mwanamageuzi kwa pamoja, sera zake za uchumi zilikuwa si za kuaminika wakati wa kapeni.
Majuzi, alilinganisha vita vyake dhidi ya walanguzi wa mihadarati na mauaji ya Wayahudi wakati wa Vita Vikuu vya Pili vya Dunia.
Alisema anaweza kuua walanguzi wengi wa dawa hizo za kulevya sawa na alivyofanya Hitler akiua Wayahudi.
"Hitler aliua Wayahudi milioni tatu ... kuna waraibu milioni tatu wa dawa za kulevya. Ninaweza kufurahia sana kuwaua," amesema.
Wayahudi zaidi ya milioni sita waliuawa na Wanazi chini ya Hitler.

No comments:

Post a Comment