Monday 24 October 2016

Kongamano la mabadiliko ya uendeshaji wa klabu za soka

football
Kongamano la mabadiliko ya uendeshaji wa klabu za soka limefanyika Jumamosi Oktoba 22, 2016 kwenye ukumbi wa Uwanja Mkuu wa Taifa, Dar es Salaam.
Kongamano hilo lililoandaliwa na chama cha Waandishi wa Habari za Michezo Tanzani (TASWA) lilishirikisha wadau zaidi ya 60 nchini.
Kituo cha televisheni cha Azam kilionesha live (mubashara) kongamano hilo huku wajumbe wakikubaliana masuala kumi ya msingi.
Kwanza wajumbe walikubali kuwa kuna umuhimu wa kufanya mabadiliko sasa kwa sababu muundo unaotumika kuendesha klabu za soka una matatizo mengi.
Pili iliamuliwa klabu zijiandae vya kutosha kukaribisha mabadiliko hayo ikiwa ni pamoja na kuboresha utawala bora (governance) kwenye uendeshaji wa klabu.
Tatu mifumo yetu kama nchi inawezesha klabu kuwa na aina nyingi za mifumo ya kiuendeshaji hivyo wanachama waelimishwe kwa kina kuhusu mifumo hiyo ili wachague ulio bora zaidi kwa manufaa ya klabu zao.
Nne ili mabadiliko haya yafanyike kwa haki, inatakiwa wamiliki wa timu hizi (wanachama) waelimishwe  vya kutosha juu ya thamani yao ili wajitambue. Kwamba thamani ya klabu kubwa nchini haiwezi kulinganishwa na kiasi cha fedha kinachotolewa na wawekezaji hivyo wanachama wasiingie kwenye mabadiliko wakiwa wanyonge kwa sababu wao ndio wana mtaji mkubwa kuliko hela zinazoletwa kwa ajili ya uwekezaji.
Tano mabadiliko haya hayawezi kufanywa na wanachama na wawekezaji pekee bila kuishirikisha serikali. Hivyo klabu zinapojipanga kwa mabadiliko haya zihakikishe zinashirikisha serikali na Shirikisho la Soka Tanzania (TFF).
Sita mabadiliko haya yasifanywe kishabiki bali yafanywe kitaalamu ili  kutengeneza msingi Imara utakaoepusha migogoro hapo baadaye.
Saba kuelekea mabadiliko haya, hasa katika kipindi hiki ambacho uelewa wa wanachama ni mdogo, serikali inatakiwa kulinda maslahi ya walio wengi kwa kuingilia kati pale inapoona kuna mwelekeo wa kuwa na mabadiliko yanayominya maslahi ya walio wengi.
Nane mpira ni biashara ya kipekee ambayo mafanikio yake yanategemea jinsi washindani wanavyoshirikiana. Hivyo kuelekea mabadiliko haya wanatakiwa watumike wataalamu wa biashara ya mpira ili klabu zinapobadilika ziweke misingi itakayokubaliana na biashara ya soka.
Tisa  klabu zinao wajibu wa kulinda hadhi zake (brand) kwa sababu eneo hilo ndio msingi wa biashara ya mpira. Hivyo klabu zinapoelekea kwenye mabadiliko, lazima zizingatie hadhi zao zinalindwaje.
Kumi Chama cha Waandishi wa Habari na Michezo kiliombwa kufanya makongamao zaidi hasa kuhusiana na aina ya mabadiliko ambayo klabu zinaweza kuingia kwa sababu inaonekana wanachama ambao ndio wamiliki wa klabu hizi hawana uelewa wa kutosha hivyo inawapunguzia wigo wa kuchagua aina ya mabadiliko.

No comments:

Post a Comment