
Kikosi cha Mabingwa
wa Tanzania bara Yanga, leo usiku saa 2:30 kinashuka uwanjani kupambana
na Jamhuri ya Pemba katika mchezo wake wa kwanza wa michuano ya Kombe
la Mapinduzi inayoendelea kutimua vumbi Visiwani Zanzibar katika Uwanja
wa Amaan ulipo mjini Unguja na mchezo wa kwanza wa kundi hilo B
utachezwa mapema saa 1:00 jioni kati ya Azam FC dhidi ya Zimamoto.
Katika mchezo huo,
Yanga imepanga kutumia majembe yake yote ili iweze kuibuka na ushindi
utakaoiwezesha kukaa kwenye mazingira mazuri ya kusonga mbele katika
michuano hiyo ambayo inashirikisha timu tisa.
Kocha msaidizi wa
timu hiyo, Juma Mwambusi, amesema kuwa wamejipanga vilivyo kwa ajili ya
mchezo huo kuhakikisha wanapata ushindi mnono ili waweze kujitengenezea
mazingira mazuri ya kusonga mbele kwenye michuano hiyo.
Alisema katika
kuhakikisha hilo linafanikiwa, wanatarajia kutumia kikosi chao kilekile
ambacho wamekuwa wakikitumia katika michuano ya Ligi Kuu Bara.
“Tupo visiwani hapa
kwa kazi moja tu ya kuhakikisha tunafanya vizuri katika mechi zetu zote,
hatuangalii timu tutakayokutana nayo, iwe Simba au Azam sisi tutaingia
uwanjani kuhakikisha tunapata matokeo na tutakuwa tukipanga kikosi cha
ushindi.
“Tumejiandaa vizuri
kwa ajili ya mechi hiyo, wachezaji wote wapo vizuri, hatuna majeruhi
hata mmoja, hivyo tunamshukuru Mungu kwa hilo,” alisema Mwambusi.
No comments:
Post a Comment