Tuesday 24 May 2016

Mipira ya kondomu yatolewa bure mitaani Rwanda

Rwanda

Vibanda vimewekwa  katika mitaa yenye viwango vya juu vya maambukizi
Nchini Rwanda, mipira ya kondomu imeanza kutolewa bure katika baadhi ya mitaa jijini Kigali ambayo inaaminika kuwa imekithiri kwa ukahaba na kuwa na idadi kubwa ya walioambukizwa virusi vya Ukimwi.
 

Vibanda vidogo vimewekwa katika mitaa hiyo kwa ajili ya huduma hiyo inayopatikana kwa saa 24.
Wizara ya afya ya Rwanda inasema asilimia 3 wa wananchi wanaishi na virusi vya Ukimwi na kwamba zoezi hilo litasaidia kupunguza kasi ya uambukizaji.

“Tulishuhudia watu wanaoacha kutumia mipira ya kondomu kwa sababu wameikosa, tukaamua kuleta hivi vibanda katika mitaa hii minne ya jiji la Kigali yenye kiwango cha juu cha maambukizi ya virusi vya Ukimwi,” anasema Dkt Sabin Nsanzimana, mmoja wa wanaohusika katika mpango huo.

“Kwa hiyo naamini tutafanikiwa kupunguza kasi ya maambukizi.”
  • Mfumo wa kisasa wa uchukuzi wazinduliwa Rwanda
Wizara ya afya ya Rwanda inasema imekuja na mbinu hii mpya ya kusambaza kondomu kwa bure baada ya kuona kwamba baadhi ya watu hushindwa kumudu bei ya kawaidia ya kondomu na wengine kuona haya kununua kondomu hadharani.

Bei ya kondomu kwenye maduka imekuwa kati ya Franka 300 na 500 za Rwanda ambazo ni karibu nusu dola ya Kimarekani.


 Rwanda
Rwanda inapanga kusambaza kondomu milioni moja mwaka huu
Kupitia mpango huu Rwanda inalenga kusambaza mipira ya kondomu milioni moja ifikapo mwishoni mwa mwaka huu.

Mwandishi wa BBC aliyepo Rwanda Yves Bucyana anasema miaka 5 iliyopita Rwanda ilijaribu mpango ambao haukufanikiwa wa kusambaza kondomu kwa kutumia mashine zilizowekwa katika sehemu za burudani.

Ili kupata kondomu ilibidi kutumbukiza vichele ndani ya mashine hizo ambazo katika sehemu nyingi sasa zimekwishaharibika.

No comments:

Post a Comment