Saturday 20 December 2014

KILIMO CHA UMWAGILIAJI KUCHANGIA ASILIMIA 25 YA CHAKULA

Waziri wa Kilimo Chakula na Ushirika, Mheshimiwa Eng.  Christopher Kajoro Chiza (Mb) ameeleza  kuwa, kilimo cha umwagiliaji  kina nafasi ya kuchangia asilimia 25 ya chakula  kinachozalishwa nchini.  Aliyalisema hayo wakati  alipotembelea mradi wa umwagiliaji wa Nkoanrua katika Halmashauri ya  Wilaya ya  Meru.
Azma hiyo inaweza kufikiwa kwa  kuongeza eneo,   pamoja na kuongeza tija katika maeneo yaliyopo. Hatua za kuchukua ni pamoja na kubadili kilimo cha kujikimu kuwa cha kibiashara.
Alisisitiza kuwa hatua hiyo itafikiwa endapo wakulima watabadilika na  kulima kilimo cha kisasa badala ya  kilimo cha mazoea.
Hatua nyingine ni kukarabati na kuisafisha mifereji  ya umwagiliaji iliyopo kwa lengo la kupunguza upotevu wa maji ili kuleta ufanisi katika matumizi ya maji.  Vile vile aliwahimiza wakulima kuzalisha mara mbili katika msimu, aliongeza Mheshimiwa Chiza.
Aidha, alihimiza umuhimu wa kulinda vyanzo vya maji na kuwa na Kamati ya watumia maji ili kuboresha huduma za umwagiliaji.
Hatua hizo zitawezesha kufikiwa kwa malengo ya Matokeo Makubwa Sasa (BRN) ambapo ifikapo  mwaka 2015 kuwe  na ongezeko la mavuno  kwa  zao la mahindi la tani 100,000, mchele tani 290,000 na Sukari tani 150,000.

No comments:

Post a Comment