Monday 15 December 2014

Watanzania tuongeze juhudi kuinua Kiswahili

 



Kwa ufupi:                                                                                                                                                  

Kwa Watanzania wazalendo wanaolipenda taifa lao hawakutakiwa kutumia Kiswahili kibovu.Hali hii ilileta aibu kwa taifa letu kwani Redio One inasikilizwa na watu wengi hata nje ya mipaka yetu                               

Lugha ya Kiswahili imekuwa ikiharibiwa siyo tu na waandishi wa habari, bali pia na wazungumzaji, hasa watangazaji wa redio na runinga.
Hivi karibuni nilikuwa na fursa ya kusikiliza majadiliano katika vyombo vyetu vya habari kuhusu Ripoti ya Escrow iliyotayarishwa na Kamati ya Bunge ya Hesabu za Mashirika ya Umma (PAC). Ilitarajiwa kuwa majadiliano haya yangetoa picha kamili kuhusu kilichojiri katika matumizi ya fedha zilizohifadhiwa katika Benki Kuu kutokana na mzozo wa kifedha kati ya Shirika la Tanesco na IPTL.
Kwa kweli wananchi wengi hawajui kwa undani sakata hili, hivyo kuwepo kwa kipindi katika redio zetu kunakuwa ni hatua nzuri ya kuielimisha umma.
Suala la escrow liligusa hisia za watu wengi wa vijijini na mijini na walikuwa na hamasa kubwa kujua kilichoendelea bungeni.
Vikundi vya watu vilikusanyika kando ya redio na runinga katika maeneo mengi nchini. Kwa hiyo kutoa ufafanuzi wa kina kulisaidiia wananchi kupata ukweli ya mambo yaliyokuwa yakiendelea bungeni.
Kinyume cha matarajio ya wengi, mjadala uliofanyika tarehe 29/11/2014 kuanzia saa sita mchana hadi saa sita na tano na dakika 49 usiku ulikuwa ni aibu tupu.
Ulikuwa ni wa aibu kwa sababu kilichojadiliwa hakikueleweka na kilikuwa ni upotoshaji uliokithiri.
Niseme tu kuwa Redio One ni redio inayoaminika sana hapa nchini, pia nchi za nje kwa kutoa taarifa za matukio mengi muhimu. Ilitarajiwa kuwa ingeweka heshima ya taifa letu kwa kuwa mfano mzuri wa kutumia lugha sanifu na fasaha kwani Kiswahili ni lugha ya taifa la Tanzania na lugha rasmi katika mawasiliano. Hata hivyo, wazungumzaji walijieleza kwa kutumia Lugha ya Kiswahili iliyochanganyika na Kiingereza.
Kwa Watanzania wazalendo wanaolipenda taifa lao hawakutakiwa kutumia Kiswahili kibovu. Hali hii ilileta aibu kwa taifa letu kwani Redio One inasikilizwa na watu wengi hata nje ya mipaka yetu.
Endapo watumiaji wa Kitanzania watatumia Kiswahili kibovu itakuwa ni aibu kwa taifa. Nitatoa mifano michache ili kuthibitisha malalamiko yangu.
Ningependa kuyahifadhi majina ya wahusika yaani mtangazaji na mzungumzaji na kijikita zaidi katika mazungunzo yao.
Mjadala uliokuwa ukiendelea, ulitumia Kiswahili kilichochanganywa na Kiingereza, hali ambayo msikilizaji wa kawaida hangeweza kuelewa kilichokuwa kikiendelea huko bungeni. Kwa maoni yangu msikilizaji wa kawaida ambaye yuko kijijini, elimu iliyokusudiwa kutolewa ingemsaidia kujifunza mambo mengi yanayoendelea nchini, lakini waliambulia patupu. Majadiliano yaliyokuwa yakifanyika yalikuwa na miundo ya sentensi kama ifuatavyo: Nafikiri this time masuala ya utaifa yaliwekwa pembeni.

No comments:

Post a Comment