Saturday 20 December 2014

Uzembe kama huu Mv Victoria usirudiwe


MV Victoria 

Jana katika gazeti hili tulichapisha habari iliyokuwa ikielezea watumiaji wanaotegemea meli ya Mv Victoria, Jumatano walipata adha ya usafiri baada ya kusitishwa kwa safari ya kuelekea Mwanza, hatua iliyochukuliwa na Mamlaka ya Udhibiti wa Usafiri wa Majini na Nchi Kavu (Sumatra) kwamba ilitoroshwa bila kukaguliwa.
Habari hiyo ilimkariri Ofisa Mfawidhi wa mamlaka hiyo mkoani Kagera, Kapteni Alex Katama akisema awali, meli hiyo ilizuiliwa Mwanza kwa ajili ya matengenezo na kwamba haikufanyiwa ukaguzi kabla ya kuruhusiwa na akisisitiza kuwa meli hiyo bado mbovu.
Ilielezwa kuwa ilipofika Bukoba ikitumia injini moja bila ruhusa ya mamlaka, waliizuia mpaka itakapofanyiwa ukaguzi na kujiridhisha.
Hadi inazuiliwa, ilikuwa ikijiandaa kwa safari hiyo ya Mwanza na tayari mizigo ilikuwa imeshapakiwa.
Hata hivyo, Meneja Masoko wa Shirika la Huduma za Meli, Obed Tirugumila alikaririwa akisema kuwa Mv Victoria ilifanyiwa matengenezo Mwanza, lakini haikufanyiwa majaribio na maofisa wa ukaguzi wa Sumatra akidai kuwa walisema hawana nafasi.
Hivyo, waliamua kufanya majaribio kwa kwenda Bukoba wakiwa na abiria na kufika salama.
Ni miaka 18 sasa tangu Meli ya Mv Bukoba izame ndani ya Ziwa Victoria Mei 21, 1996 ikitokea Bandari ya Bukoba kwenda Bandari ya Mwanza na kuua zaidi ya watu 1,000 kutokana na kuzidisha mizigo na abiria.
MV Bukoba ilizama ikiwa imebakisha umbali mfupi kufika Bandari ya Mwanza, lakini ukosefu wa vifaa vya uokoaji vilisababisha kuongezeka idadi ya watu waliokufa.
Waokoaji wa ajali hiyo walisubiriwa kufika nchini kutokea Afrika Kusini, ambao waliweza kuogelea na kuokoa baadhi ya maiti chache zilizokuwa zimezama umbali wa mita 25 chini ya maji.
Serikali ilimshtaki aliyekuwa nahodha wa Mv Bukoba, Jumanne Rume-Mwiru, (sasa marehemu), Mkaguzi wa Mamlaka ya Bandari Gilbert Mokiwa; aliyekuwa Meneja wa Bandari ya Bukoba, Alphonce Sambo na aliyekuwa Maneja wa Bandari ya Kemondo, Prosper Lugumila.
Kama hiyo haitoshi, mwaka 2011 ajali nyingine mbaya ya Meli ya Spice Islander iliyokuwa inatoka Dar es Salaam kwenda Pemba ilizama na kuua watu 240.
Tume iliyochunguza ajali ya meli hiyo ilisema meli hiyo ilibeba zaidi ya abiria 2,000 ingawa maelezo ya nahodha wa meli alidai kuwa melini kulikuwa na watu 500.

No comments:

Post a Comment