Wednesday 29 March 2017

Ronaldo apewa uwanja wa Ndege

Cristiano Ronaldo alifunga bao kwenye mechi iliyochezewa katika kisiwa alikozaliwa cha Madeira, siku moja kabla ya uwanja wa ndege katika eneo hilo kupewa jina lake.
Ureno hata hivyo, walitupa uongozi wa mabao mawili na mwishowe wakalazwa 3-2 na Sweden.
Ureno walikuwa wanaongoza kupitia bao la 71 la Ronaldo katika michuano ya kimataifa, pamoja na bao la kujifunga na Andreas Granqvist.
Lakini Viktor Claesson alifunga mawili naye Cavaco Cancelo kajifunga dakika za mwisho mwisho na kuwapa Sweden ushindi.
Ronaldo anatarajiwa kuhudhuria sherehe ya kuupa uwanja huo jina lake leo Jumatano.
Ronaldo, 32, anayechezea Real Madrid, aliongoza taifa lake kushinda ubingwa wa Ulaya mwaka jana.
Alizaliwa katika mji mkuu wa Madeira, Funchal na baadaye akachezea Sporting Lisbon na Manchester United.
Baadhi ya wanasiasa wa eneo hilo wamepinga uamuzi wa kubadilisha jina la uwanja wa ndege wa Madeira kuwa Uwanja wa Ndege wa Cristiano Ronaldo.
"Wakati mwingine, shukrani za taifa huwa hazidumu sana, lakini Madeira haitasahau," Miguel Albuquerque, rais wa serikali ya Madeira alitangaza, hatua ya kubadilisha jina la uwanja huo ilipotangazwa.
Funchal tayari ina sanamu ya Ronaldo pamoja na makumbusho.
Kuna pia hoteli kubwa iliyopewa jina la nahodha huyo wa Ureno.
Jumanne jioni ilikuwa mara yake ya kwanza kwa Ronaldo kuchezea kisiwa chake cha kuzaliwa akichezea Ureno.
 
Alizunguka uwanja akiwa na Kombe la Ulaya kabla ya mechi kuanza.
Sherehe hata hivyo zilitiwa mchanga kwa kulazwa na Sweden ambao sasa wameshinda mechi tatu mtawalia za kimataifa.
Ureno na Sweden wamo nafasi ya pili katika makundi yao ya kufuzu kwa Kombe la Dunia.

No comments:

Post a Comment