Wednesday 22 March 2017

Manchester City na Manchester United kukutana kwa Trump

Manchester City watakutana na Manchester United katika mechi ya kirafiki ya kujiandaa kwa msimu nchini Marekani tarehe 20 Julai.
Uwanja utakaochezewa mechi hiyo bado haujaamuliwa.
Mechi hiyo, debi ya kwanza ya Manchester kuchezewa nje ya Uingereza, itachezwa kama sehemu ya michuano ya kila mwaka ya Kombe la Mabingwa wa Kimataifa.
City walifaa kukutana na United jijini Beijing, Uchina Julai mwaka jana katika uwanja wa Bird's Nest lakini mechi hiyo ikafutiliwa mbali kutokana na mvua kubwa.
City pia watakabiliana na wapinzani wao wengine kutoka Ligi ya Premia, Tottenham, mjini Nashville 29 Julai kabla ya kukabiliana na miamba wa Uhispania Real Madrid mjini Los Angeles 26 Julai.
Spurs pia watakutana na mabingwa wa Ufaransa Paris St-Germain, ambao wameshinda michuano hiyo miaka miwili iliyopita, mjini Orlando 22 Julai na Roma ya Italia New Jersey 25 Julai.
Kwenye mechi hiyo, kutachezwa pia El Clasico ya pili kuwahi kuchezewa nje ya Uhispania, Real Madrid watakapokutana na Barcelona Miami 29 Julai.
Timu hizo zilikutana mara ya mwisho nje ya Uhispania Venezuela mwaka 1982.

United pia watakutana na Real Madrid mjini Santa Clara 23 Julai kisha wakutane na Barcelona Washington DC mnamo 26 Julai.

Kwenye mechi nyingine za Kombe la Mabingwa wa Kimataifa zitakazochezewa Singapore, viongozi wa Ligi Kuu England Chelsea watacheza dhidi ya mabingwa wa Ujerumani Bayern Munich 25 Julai na Inter Milan ya Italia 29 Julai.

Arsenal watashiriki mechi zitakazochezewa China.

No comments:

Post a Comment