Waziri wa Nishati na Madini
Profesa Sospeter Muhongo (kulia) akielezea fursa za uwekezaji katika
Sekta ya Nishati kwa Balozi wa Uingereza Nchini, Sarah Cooke (kushoto).
Balozi wa Uingereza Nchini,
Sarah Cooke akielezea mikakati ya nchi yake katika kuisaidia Tanzania
katika uboreshaji wa sekta ya nishati nchini.
Watendaji kutoka kutoka Wizara
ya Nishati na Madini, Shirika la Maendeleo ya Petroli Nchini (TPDC),
Shirika la Umeme Nchini (TANESCO), Mamlaka ya Udhibiti wa Huduma za
Nishati na Maji (EWURA), Wakala wa Nishati Vijijini (REA) na Wakala wa
Ukaguzi wa Madini Nchini (TMAA), wakifuatilia maelezo yaliyokuwa
yanatolewa na Waziri wa Nishati na Madini Profesa Sospeter Muhongo
(hayupo pichani).
Balozi wa Uingereza Nchini,
Sarah Cooke (kushoto) akisaini kitabu cha wageni kwenye ofisi ya Waziri
wa Nishati na Madini Profesa Sospeter Muhongo.
Waziri wa Nishati na Madini
Profesa Sospeter Muhongo (kulia) akibadilishana mawazo na Balozi wa
Uingereza Nchini, Sarah Cooke (kushoto) mara baada ya kumalizika kwa
mazungumzo ofisini kwake.
Waziri wa Nishati na Madini
Profesa Sospeter Muhongo (kulia) na Balozi wa Uingereza Nchini,
Sarah Cooke (kushoto) wakiwa katika picha ya pamoja.
Na Greyson Mwase, Dar es Salaam
Balozi wa Uingereza Nchini,
Sarah Cooke amemtembelea Waziri wa Nishati na Madini Profesa Sospeter
Muhongo jijini Dar es Salaam lengo likiwa ni kujadili namna Serikali
ya Uingereza inavyoweza kufanya kazi na Tanzania kwenye uboreshaji wa
sekta za Nishati na Madini.
Balozi Cooke alifanya mazungumzo
na Profesa Muhongo pamoja na Watendaji kutoka Wizara ya Nishati na
Madini, Shirika la Maendeleo ya Petroli Nchini (TPDC), Shirika la Umeme
Nchini (TANESCO), Mamlaka ya Udhibiti wa Huduma za Nishati na Maji
(EWURA), Wakala wa Nishati Vijijini (REA) na Wakala wa Ukaguzi wa
Madini Nchini (TMAA)
Akielezea kuhusu Sekta ya
Nishati nchini, Profesa Muhongo alisema kuwa Serikali imeweka mikakati
ya matumizi ya vyanzo vya nishati ya umeme kama vile gesi, maji,
jotoardhi, makaa ya mawe, upepo, jua na kukaribisha wawekezaji kutoka
Uingereza kushirikiana na Serikali kwenye uzalishaji na usambazaji wa
umeme nchini hususan katika maeneo ya vijijini.
Aliongeza kuwa, Serikali imeanza
kutumia gesi yake iliyogunduliwa kwa wingi kwa kiwango cha futi za
ujazo trilioni 57.2 kwa kujenga bomba la gesi kutoka Mtwara hadi jijini
Dar es Salaam na kuendelea kusema kuwa Serikali imeweka mkakati wa
kusambaza gesi mikoani pamoja na nyingine kuuzwa nje ya nchi.
“Kuna nchi zilizopo Ukanda wa
Afrika Mashariki zimeomba bomba la gesi liende kwao; hii itatuwezesha
sisi kufanya biashara pamoja nao na kuingiza fedha za kigeni,” alisema
Profesa Muhongo
Aliongeza kuwa, mikakati mingine inayofanywa na Serikali ni pamoja na ujenzi wa kiwanda cha kusindika gesi kimiminika ( Liquefied Natural Gas Plant) na kiwanda cha mbolea katika eneo la Kilwa mkoani Lindi na kiwanda kingine cha mbolea katika mkoa wa Mtwara.
Alisisitiza kuwa, bado Serikali
inaendelea na shughuli za utafutaji wa mafuta na gesi katika maeneo
mbalimbali nchini na kuomba kampuni za Uingereza zenye uzoefu kujitokeza
na kuwekeza nchini.
Aidha, Profesa Muhongo alimwomba
Balozi wa Uingereza kusaidia nchi ya Tanzania katika uendelezaji wa
rasilimaliwatu kupitia nafasi za ufadhili zinazotolewa na ubalozi huo
kwa ajili ya kusomea shahada ya uzamifu katika masuala ya sheria na
uzimamizi katika sekta za gesi na mafuta.
Naye, balozi wa Uingereza
Nchini, Sarah Cooke alisema serikali yake inaunga mkono juhudi za Rais
wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dk. John Pombe Magufuli ya kufanya
Tanzania kuwa nchi ya viwanda na kumhakikishia Waziri, kuwa
atashawishi kampuni za Uingereza kuwekeza kwenye sekta za nishati na
madini.
No comments:
Post a Comment