Tuesday 28 July 2015

“Watanzania wanataka mabadiliko...watayatafuta nje ya CCM"




Hayati Baba wa Taifa, Mwalimu Nyerere


Dar es Salaam. Kauli ya hayati Baba wa Taifa, Mwalimu Nyerere kuwa Watanzania wanataka mabadiliko na wasipoyapata ndani ya CCM, watayatafuta nje ya CCM inaweza kutimia mwaka huu.
Mwalimu alikuwa akihutubia Mkutano Mkuu wa Halmashauri Kuu ya CCM mkoani Dodoma wakati wa mchakato wa kumpata rais wa awamu ya tatu mwaka 1995. Alisema mambo mengi lakini aliwasisitizia wajumbe kuwa Watanzania wanataka mabadiliko na kwamba wasipoyapata ndani ya CCM, watayatafuta nje ya CCM.
Huku akisikilizwa kwa umakini, Mwalimu alisema kuna mambo Watanzania wanataka uongozi wa awamu ya tatu uyafanye mojawapo ni kupambana na rushwa kwa kuwa Watanzania wengi wamechoka na rushwa.
“Wajumbe wa zamani wa NEC watakumbuka nimepigia sana kelele rushwa wakati nikiwa mwenyekiti. Sasa hivi hali ya rushwa ni mbaya.”
Aliongeza; “Pili, Tanzania ni masikini, nchi ni ya wakulima na wafanyakazi ambao si matajiri, nchi haijawa ya matajiri, chama hakijawa chama cha matajiri, tushughulikie kwa dhati matatizo ya wananchi, hali zao za uchumi, viwandani, mashambani, shuleni, hospitalini na ateuliwe mtu ambaye anajua nchi bado ya masikini, wakulima na wafanyakazi na awe anatambua hivyo.”
Suala la tatu alilozungumzia ni kuhusu udini akisema umeanza kuzungumzwa kama vile ni sifa. Alisema zamani hawakuwa wanazungumzia udini wala kujali dini ya mtu kwa vile ni ya mtu mwenyewe anaijua na hawakuwa wanauliza dini ya mtu, kwa kuwa haiwahusu.
“Tunataka nchi yetu ipate kiongozi safi, na kiongozi safi hawezi kutoka nje ya CCM, ninyi wapiga kura, mnaweza kutupatia kiongozi safi kwa kura zenu, sasa tupatieni kiongozi safi.”

No comments:

Post a Comment