Wednesday 29 July 2015

CCM yaonya vijana kubeza wagombea wake.


Chama Cha Mapinduzi (CCM)
Katibu Mwenezi wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) Wilaya ya Songea Mjini mkoani Ruvuma, Marco Mbawala, amewaonya baadhi ya vijana wanaosadikiwa kuwa wanachama wa vyama vya upinzani  kuacha kuwakejeli wagombea ubunge wa Jimbo la Songea mjini kwa tiketi ya CCM ili kuepusha vurugu na kuharibu mchakato wa uchaguzi ndani ya chama hicho.
 
Onyo hilo alilitoa juzi baada ya baadhi ya vijana hao kuwauliza maswali ya kejeli wagombea ubunge hao, wakati wakijinadi kwenye mikutano ya chama hicho katika kata za Mshangano, Msamala na Bombambili.
 
Marko alisema wagombea hao wanaomba ridhaa kwa wanaCCM  ili apatikane mmoja wao wa kupeperusha bendera ya chama hicho katika Uchaguzi Mkuu utakaofanyika nchini Oktoba 25, mwaka huu.
 
Alisema wanachama wa vyama vingine hawana ruhusa ya kuwauliza maswali wagombea wa CCM bali wasubiri atakapopatikana wa kupambana na atakayechaguliwa kutoka vyama vingine vya upinzani.
Vilevile  katibu huyo amewataka wanachama wa chama hicho kuacha tabia za kuuliza maswali ya kupandikizwa wagombea hao bali wafanye hivyo kwa kwa utashi wao.
 
Wagombea hao ni Leonidas Gama (Mkuu wa mkoa Kirimanjaro), Francis Miti (Mkuu wa Wilaya ya Hanang’  mkoani Arusha), Theresia Uvisa ambaye (alikuwa mbunge viti maalum kupitia vyuo vikuu vishiriki na Waziri wa Mazingira),  Azizi Mohamed (Katibu wa CCM Namtumbo), Sebastian Waliyuba (Wakili wa kujitegemea).
 
Wengine ni Erick Mapunda (Mhadhiri wa Chuo kikuu cha Sayansi na Teknolojia Mbeya) ,Raymond  Mhenga (Ofisa Masoko wa Claus FM) na  Mussa Gama ambaye ni mtoto wa Marehemu Lawrence Gama (Katibu Mstaafu wa CCM ). 

No comments:

Post a Comment