Kaimu Msajili wa Mabaraza ya
Ardhi na Nyumba ya Wilaya, Bibi. Amina Rashid Ntibampemba akizungumza na
waandishi wa habari kuhusu mafanikio ya Mabaraza hayo leo Jijini Dar es
Salaam. Kulia ni Mkuu wa Kitengo cha Mawasiliano Serikalini wa Wizara
ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi Mboza Lwandiko.
Mkuu wa Kitengo cha Mawasiliano
Serikalini kutoka Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi Bi.
Mboza Lwandiko akizungumza na waandishi wa habari (hawapo pichani)
kuhusu hali ya Mabaraza ya Ardhi na Nyumba ya wilaya leo Jijini Dar es
Salaam.
Na Georgina Misama – MAELEZO
Wizara ya Ardhi, Nyumba
naMaendeleo ya Makazi imewataka watanzania kutumia Mabaraza ya Ardhi na
Nyumba ya Wilaya katika kutatua matatizo mbalimbali yanayohusu Nyumba
na Makazi.
Hayo yamesemwa leo na Kaimu
Msajili Mabaraza ya Ardhi na Nyumba ya Wilaya Bi Amina Rashidi wakati
akiongea na waandishi wa habari katika ukumbi wa Idara ya habari
Maelezo.
“Mabaraza ya Ardhi na Nyumba
ndiyo chombo pekee kilichoundwa kwa ajili ya kutatua matatizo yote
yanayohusu ardhi na nyumba” alisema Amina.
Akitaja baadhi ya mashauri
yanayosikilizwa kwenye Mabaraza hayo Amina alisema mashauri yanayotokana
na milki pandikizi (double allocation) au mashauri ya wananchi
wanaopakana kwa mmoja wao kutaka kujipanulia eneo. Yapo pia mashauri ya
wenye nyumba na wapangaji yanayofunguliwa kwa kukiukwa kwa mikataba.
Aidha, Amina alifafanua kwamba
uendeshaji wa mashauri katika Mabaraza ya Ardhi na Nyumba ni wakirafiki
nasio unaofuata taratibu za Mahakama za kawaida. Wajumbe wa Baraza
wanatoka miongoni mwa wanajamii wa eneo ambalo Baraza limeundwa.
Nae Mkuu wa Kitengo cha
Mawasiliano Serikalini kutoka Wizara ya Ardhi Nyumba na Maendeleo ya
makazi Bi. Mboza Lwandiko alitolea ufafanuzi wa dhamira ya wizara yake
katika kuhakikisha inapambana na ongezeko la mashauri kwa kuunda
Mabaraza mapya yapatayo 20 kila mwaka.
“Katika mwaka wa fedha 2016/2017
Wizara itakamilisha taratibu za kuunda Mabaraza(44) kati ya Mabaraza
mapya 47 yaliyoundwa na tangazo la serikali la mwezi Aprili, 2016”
alisema Mboza.
Tayari takribani mashauri elfu 43
yamesikilizwa kati ya mashauri elfu 59 yaliyofunguliwa kwa kipindi cha
kuanzia Oktoba 2004 na Septemba 2016.
No comments:
Post a Comment