Monday 17 October 2016

Wizara ya Ardhi, Nyumba naMaendeleo ya Makazi imewataka watanzania kutumia Mabaraza ya Ardhi na Nyumba ya Wilaya katika kutatua matatizo

maba1
Kaimu Msajili wa Mabaraza ya Ardhi na Nyumba ya Wilaya, Bibi. Amina Rashid Ntibampemba akizungumza na waandishi wa habari kuhusu mafanikio ya Mabaraza hayo leo Jijini Dar es Salaam. Kulia ni Mkuu wa Kitengo cha Mawasiliano Serikalini wa Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi Mboza Lwandiko.
maba2
Mkuu wa Kitengo cha Mawasiliano Serikalini kutoka Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi Bi. Mboza Lwandiko akizungumza na waandishi wa habari (hawapo pichani) kuhusu hali ya Mabaraza ya Ardhi na Nyumba ya wilaya leo Jijini Dar es Salaam.

Na Georgina Misama – MAELEZO
Wizara ya Ardhi, Nyumba naMaendeleo ya Makazi imewataka watanzania kutumia Mabaraza ya Ardhi na Nyumba ya Wilaya  katika kutatua matatizo mbalimbali yanayohusu Nyumba na Makazi.
Hayo yamesemwa leo na Kaimu Msajili Mabaraza ya Ardhi na Nyumba ya Wilaya Bi Amina Rashidi wakati akiongea na waandishi wa habari katika ukumbi wa Idara ya habari Maelezo.
“Mabaraza ya Ardhi na Nyumba ndiyo chombo pekee kilichoundwa kwa ajili ya kutatua matatizo yote yanayohusu ardhi na nyumba” alisema Amina.
Akitaja baadhi ya mashauri yanayosikilizwa kwenye Mabaraza hayo Amina alisema mashauri yanayotokana na milki pandikizi (double allocation) au mashauri ya wananchi wanaopakana kwa mmoja wao kutaka kujipanulia eneo. Yapo pia mashauri ya wenye nyumba na wapangaji yanayofunguliwa kwa kukiukwa kwa mikataba.
Aidha, Amina alifafanua kwamba uendeshaji wa mashauri katika Mabaraza ya Ardhi na Nyumba ni wakirafiki nasio unaofuata taratibu za Mahakama za kawaida. Wajumbe wa Baraza wanatoka miongoni mwa wanajamii wa eneo ambalo Baraza limeundwa.
Nae Mkuu wa Kitengo cha Mawasiliano Serikalini kutoka Wizara ya Ardhi Nyumba na Maendeleo ya makazi  Bi. Mboza Lwandiko alitolea ufafanuzi wa dhamira ya wizara yake katika kuhakikisha inapambana na ongezeko la mashauri kwa kuunda Mabaraza mapya yapatayo 20 kila mwaka.
“Katika mwaka wa fedha 2016/2017 Wizara itakamilisha taratibu za kuunda Mabaraza(44) kati ya Mabaraza mapya 47 yaliyoundwa na tangazo la serikali la mwezi Aprili, 2016” alisema Mboza.
Tayari takribani mashauri elfu 43 yamesikilizwa kati ya mashauri elfu 59 yaliyofunguliwa kwa kipindi cha kuanzia Oktoba 2004 na Septemba 2016.

No comments:

Post a Comment