Monday 2 February 2015

Wabunge: Kitengo cha deni la Taifa kinahitaji wataalamu



Dodoma. Wabunge wameitaka Serikali kutofanya haraka kuanzisha kitengo cha deni la Taifa hadi hapo kutakapokuwa na wataalamu wenye weledi wa kutosha.
Walisema hayo juzi katika semina ya Kamati ya Bunge ya Uchumi, Viwanda na Biashara iliyoandaliwa na Taasisi ya Tanzania Coalition on Debt Development (TCDD).
Makamu Mwenyekiti wa kamati hiyo, Dutsun Kitandula alisema deni hilo limesemwa na wananchi kwa muda mrefu na kwamba wabunge nao wana wajibu wa kulijadili.
“Tusifanye haraka, ni lazima tujifunze na kujipa muda wa kupata wataalamu,” alisema Kitandula.
Mbunge wa Viti Maalumu (Chadema), Cecilia Pareso alisema Serikali inapotaka kukopa, lazima ieleze ni kiasi gani inakopa, italipa lini na riba ni kiasi gani.
“Kwa sababu Taifa linapokopa, kila mtu anadaiwa kama siyo leo, basi ni kizazi kijacho,” alisema Pareso.
Mbunge wa Nkasi (CCM), Ally Keissy alisema deni hilo limekuwa kubwa kwa sababu Serikali huwapa dhamana wafanyabiashara waliofilisika.
“Fedha zenyewe hazikusaidia wananchi wala kujenga barabara, Taifa halikunufaika pia,” alisema Keissy.
Mkurugenzi Mtendaji wa TCDD, Heribon Mwakagenda alisema deni la Taifa limefikia Sh30 trilioni.
Alisema: “Ni bora wakati mnatunga sheria kuwe na udhibiti zaidi.
“Serikali ikiomba kibali inapotaka kukopa, lakini kuwe na kikomo ambacho nchi haiwezi kukopa tena,” alisema.

No comments:

Post a Comment