Kwa nini si Hilary Clinton? Ndilo swali ambalo linaulizwa kila kona
baada ya mgombea huyo wa chama cha Democtratic kuangushwa na Donald
Trump wa Republican katika Uchaguzi Mkuu wa Marekani.

Si rahisi kuamini Clinton kushindwa na mgombea ambaye alikuwa akihubiri
sera za kibaguzi na kujenga hofu kwa baadhi ya makundi ya Wamarekani.
Wamarekani wenye asili ya Afrika na Wamexico walionekana kuwa wanamuunga
mkono mke huyo wa Rais wa 42 wa Taifa hilo kubwa ulimwenguni.
Kura zao zilionekana kuwa zingeongeza idadi katika kura za raia wengine
wa Marekani waliokuwa wanamuunga mkono mgombea huyo wa chama tawala kwa
sasa. Lakini baada ya Trump kupata ushindi, maelezo ya kuhalalisha
matokeo hayo yanayoshangaza yanaweza kueleweka.
Kwa kawaida, si rahisi kwa chama kilicho madarakani kushinda tena
uchaguzi baada ya miaka minane ya vipindi viwili vya urais ukiondoa
wakati George H.W. Bush alipoongoza kwa vipindi viwili na kupokelewa na
Ronald Reagan, kitu ambacho ni cha kipekee.
Pamoja na utamaduni huo wa kupokezana madaraka baada ya miaka minne,
kuna sababu kuu tano zinazoweza kueleza kwa nini Trump, bilionea maarufu
Marekani na mtangazaji wa kipindi cha Apprentice, amefanikiwa
kumuangusha Clinton aliyeonekana kuelekea kuweka historia ya kuwa
mwanamke wa kwanza kuongoza taifa hilo.
Kushindwa kuunganisha makundi
Moja ya sababu kuu ya kuanguka kwa waziri huyo wa mambo ya nje ni
kushindwa kuendeleza nguvu ya rais wa sasa, Barack Obama ya kuunganisha
makundi ya wananchi wa Marekani.
Wamarekani wenye asili ya Afrika, ya Amerika Kusini na wapiga kura
vijana hawakujitokeza kwa wingi kupiga kura kuweza kumuingiza Ikulu
Clinton.
Kabla ya matokeo kutangazwa, alikuwa na uhakika wa ushindi. Lakini
mwishoni alijikuta akianguka kwenye majimbo yaliyoonekana yako nyuma
yake, kama Wisconsin. Aliachwa kwenye majimbo mengine kama Pennsylvania
na Michigan.
Wakati alikusanya kura nyingi kutoka kwenye makundi yenye watu wengi
ambayo kampeni zake ziliyalenga, hakuweza kufikia idadi ambayo Obama
alipata, hata miongoni mwa wanawake.
Idadi kubwa kidogo ya Wamarekani weusi na Walatino walimpa kura nyingi
Trump kuliko walivyompigia Mitt Romney kwenye uchaguzi wa mwaka 2012,
licha ya kauli zake kali kwa Wamarekani wenye asili ya Afrika, Wamexico
na wahamiaji wasio na nyaraka.
Obama, ambaye alishinda urais kutokana na msaada wa Wamarekani wenye
asili ya Afrika na jamii za Kilatino, mara kadhaa aliomba wapiga kura
weusi kumuunga mkono Clinton.
Lakini, Trump akatumia ujanja kushawishi Wamarekani weusi kwa
kuzungumzia maisha yao halisi, akisema wanaishi maisha ya kimaskini,
hawana kazi na wanauawa kila wanapotembea mitaani.
“Mtapoteza nini?” alisema katika moja ya hotuba zake.
Trump alisema maneno hayo kwenye moja ya mikutano yake ya kampeni.
“Tutajenga upya makazi ya watu wa chini kwa sababu jamii za Wamarekani
wenye asili ya Afrika wako kwenye hali mbaya sana kuliko walivyowahi
kuwa,” alisema Trump katika moja ya mikutano yake iliyohudhuriwa na
Wamarekani weupe tu.
“Angalia kwenye maeneo yao, utaona hakuna elimu, ajira na ukitembea
mitaani unauawa kwa risasi. Wako kwenye hali mbaya – namaanisha, kutoka
moyoni kabisa, nchi kama Afghanistan ni salama zaidi kuliko maeneo yao
ya sasa.”
Clinton pia hakuwa maarufu miongoni mwa watu weupe kama alivyokuwa kwa
Obama. Alipata asilimia 37 ya kura za Wamarekani weupe kulinganisha na
asilimia 39 alizopata Obama. Cha ajabu ni kwamba hata Trump alipata
asilimia chache kulinganisha na Romney (asilimia 58 kwa 59).
Idadi ya wapiga kura weupe ni asilimia 70, ikiwa imeshuka kutoka asilimia 72 miaka minne iliyopita.
Hata wapiga kura wenye asili ya Asia, ambao ni asilimia 4 tu, hawakumuunga mkono Clinton kama ilivyokuwa kwa Obama.
Wapigakura vijana pia hawakumuunga mkono Clinton na walifanya hivyo
kwenye kura za maoni ndani ya Democratic walipompa kura nyingi mpinzani
wake, Bernie Sanders na pia walipompendelea zaidi Obama miaka minne
iliyopita.
Uchumi
Pia kitendo cha Trump kuwashawishi Wamarekani kuwa sera mbovu za utawala
wa sasa na mipango mibovu ya biashara ndiyo iliyoharibu uchumi wa
Marekani. Obama alisaidia kuunusuru uchumi wa Marekani kutoka katika
janga la kuporomoka kutokana na tatizo la fedha.
Kwa bahati mbaya, kwa upande wa Clinton, Wamarekani wengi hawakuliona
hilo. Mishahara isiyopanda na kukua kwa tofauti katika jamii, ni mambo
ambayo wengi waliona yanawaathiri. Trump alifanikiwa kuwashawishi kuwa
hiyo ilitokana na mikataba mibovu ya biashara na uendeshaji mbovu wa
uchumi.
Licha ya mpinzani wake kwenye kura za maoni, Sanders kumbana katika
suala hilo, Clinton hakuonekana kuwa na jibu la kutosheleza. Sura yake
ya kinyonga katika masuala ya biashara ilionekana na baadaye
ikathibitisha na barua pepe zilizovujishwa.
Licha ya tabia ya Trump ya kutoa kauli tata na kushambulia baadhi ya
makundi kwenye jamii, Clinton alionekana kushindwa kushawishi wapigakura
kuhusu uchumi.
Ombwe la ujumbe wa Clinton
Tofauti na Obama aliyejinadi kwa kauli mbiu ya “matumaini na
mabadiliko”, ujumbe wa Clinton wa “pamoja imara” ulipendwa na wengi,
hasa wanaoiunga mkono Democratic lakini ulionekana kulenga zaidi kujibu
hotuba za kibaguzi za Trump.
Uaminifu
Tatizo jingine kubwa lililomharibia Clinton lilikuwa na ukosefu wa
uaminifu. Hotuba alizokuwa akitoa kwa malipo kwa kampuni ya kimataifa ya
Marekani inayojihusisha na uwekezaji katika benki na uongozi, Goldman
Sachs na mtandao wa mahusiano ya kibiashara kati ya taasisi ya hiari
inayomilikiwa na familia ya Clinton, iliacha Wamarekani wengi wakitia
shaka uaminifu wake kwenye masuala ya fedha.
Shaka hiyo ilifanya Ofisi ya Upelelezi ya Marekani (FBI) kufanya
uchunguzi wa mgombea huyo wa Democratic hadi siku mbili kabla ya kupiga
kura, kukiwa na matarajio ya uwezekano wa kuanzishwa kwa mashtaka ya
jinai dhidi yake.
Licha ya FBI kumsafisha dakika za mwisho, tayari ilishatia doa kuwa
mgombea huyo na mumewe walikuwa wakiendesha mambo kana kwamba sheria
haziwahusu.
Kuanguka kwa kura za maoni
Kura za maoni zafaa kuangaliwa kwa mtazamo wa pekee kutokana na
kuonyesha kuwa Clinton alikuwa anaongoza kwa pointi tatu hadi nne katika
kipindi cha kuelekea upigaji kura. Baadhi ya waendeshaji wa kura hizo
kama mtandao wa Nate Silver’s 538 ulionyesha uwezekano wa kuwepo matokeo
ya kushangaza kwenye majimbo muhimu, lakini haukumpa Trump matarajio ya
ushindi unaoweza kuzidi asilimia 30.
Kushindwa huko kwa kura za maoni kutoa picha halisi ya uchaguzi huo, kwa
kiasi fulani kunaonyesha kuanguka kwa sekta hiyo iliyojijengea sifa
kwenye chaguzi za Marekani. Mbinu ya kutafuta maoni kwa kutumia simu za
mezani, au za mkononi na utafutaji wa kisasa wa sampuli za takwimu
unaonekana kutoa matokeo yasiyo sahihi ya chaguzi kote duniani.
No comments:
Post a Comment