Tuesday 17 October 2017

Bomoabomoa yatinga Segerea

 Image result for BOMOABOMOA SEGEREA
Kikosi cha bomoabomoa chini ya usimamizi wa mgambo kimevunja nyumba tisa katika mtaa wa Mogo, njia panda ya Segerea jijini Dar es Salaam.
Wakazi katika nyumba hizo wamesema hawakupewa taarifa kwamba leo Jumanne, Oktoba 17, 2017 zingebomolewa.

Baadhi ya wapangaji katika nyumba hizo wamesema wanamtambua mmiliki lakini hawakuwa wameelezwa chochote.

“Wamekuja asubuhi saa 11:00 wakaanza kubomoa watu tumelala ndani, tunawauliza wanasema oda ya kuondoka imetolewa wiki mbili zilizopita kwa mmiliki, lakini sisi hatujui, hakuna tangazo lolote lililotolewa kwa wapangaji," amesema mpangaji aliyejitambulisha kwa jina la mama Aloyce.

Baadhi ya wapangaji wamesema mmiliki wa nyumba hizo anadaiwa na benki.

Nyumba zilizobomolewa ni za makazi ya kuishi, vyumba vya biashara na kituo kinachotumiwa na Kanisa la Moravian Ukonga.


Wakati bomoabomoa hiyo ikiendelea, aliyekuwa akisimamia kazi hiyo alitoweka, huku wengine waliohusika kubomoa hawakutaka kueleza chochote.

Askari wa Jeshi la Polisi waliofika eneo hilo hawakuwa tayari kuzungumzia tukio hilo wakisema si wasemaji.

No comments:

Post a Comment